April 25, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Baadhi ya wanafunzi wa kidato cha kwanza wa Seka Sekondar, wakiendelea na masomo darasani

Sekondari mpya Seka yaanza rasmi na wanafunzi 113

Na Mwandishi Wetu,TimesMajira Online,Mara

SHULE ya Sekondari Seka iliopo Kata ya Nyamrandirira, Musoma Vijijini mkoani Mara, ambayo imejengwa kwa nguvu za wananchi, ilifunguliwa rasmi mwezi huu ikiwa na wanafunzi 113 wa kidato cha kwanza.

Wakazi wa vijiji vitano vya Chumwi, Kaboni, Kasoma, Mikuyu na Seka kwa kushirikiana na serikali, wamekamilisha awamu ya kwanza ya ujenzi wa shule hiyo kwa kuchangia fedha taslimu na pia kutoa nguvukazi yao.

Hayo yamesemwa na Ofisa Elimu Sekondari wa Wilaya ya Musoma,Majidu Karugendo na kufafanua kuwa sekondari hiyo ilifunguliwa rasmi Julai 5 mwaka huu ikiwa na wanafunzi 113 na walimu saba.

Shule imeanza ikiwa na vyumba viwili vya madarasa,ofisi moja ya walimu, vyoo matundu 12, yakiwamo mawili ya choo cha walimu, huku juhudi zikiendelea za kuhakikisha inakamilika,” amesema Karugendo.

Amefafanua zaidi jinsi awamu ya kwanza ya ujenzi huo ilivyofanikiwa, alisema, Kijiji cha Kaboni inachangia kila kaya Sh. 10,000, Kijiji cha Seka kila kaya Sh. 15,000 hadi 20,000 na Kijiji cha Kasoma kila kaya Sh. 10,000.

“Kijiji cha Chumwi, kila kaya Sh. 6,500, Kijiji cha Mikuyu, kila kaya inachangia Tsh 20,000, Diwani wa Kata ya Nyamrandirira Nyeoja Wanjara na wa viti maalum Nyachiro Makweva wamechangia Sh. 515,000,” amesema.

Amefafanua kuwa mgodi wa MMG uliopo Kijiji cha Seka umechangia umechangia Sh. milioni 8, mawe tripu 20, molamu tripu 50, mchanga tripu 10 na utengenezaji wa barabara iendayo Seka Sekondari.

“Wazaliwa 22 wa Kata ya Nyamrandirira wamechangia jumla ya Sh. 1.9 wakati mbunge wa jimbo Prof. Sospeter Muhongo akiwa amechangia mifuko 250 ya saruji na Mfuko wa Jimbo umechangia mifuko 450 ya saruji,” amesema.

Ofisa elimu huyo amesema, Halmashauri ya Wilaya ya Musoma, imechangia Sh. milioni 5 na mifuko 50 ya saruji, wakati yeye Karugendo akiwa amechangia Sh. 60,000.

Karugendo amesema, wilaya hiyo ina kata 21 na jumla ya sekondari 22 za kata na mbili za binafsi, na kwamba mpya 10 zinaendelea kujengwa, huku myingine zaidi zikitarajiwa kuanza kujengwa