March 7, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

SanlamAllianz Yazindua Chapa Yake Mpya Tanzania

Na Agnes Alcardo, Timesmajira Online

KAMPUNI ya Bima (SanlamAllianz) imezindua rasmi chapa yake mpya nchini Tanzania, mwishoni mwa wiki, pamoja na kuwapatia mitaji wajasiriamali wanawake zaidi ya 40 katika maeneo ya Kariakoo, Makumbusho na Kawe, lengo likiwa kuwatua moyo wanawake wanaojitafutia kipato kupitia biashara ndogondogo.

Uzinduzi huu unafuatia muunganiko uliofanyika mwaka 2023 kati ya makampuni mawili makubwa ya kimataifa katika Sekta ya Bima, Sanlam na Allianz ambapo umeunda kampuni kubwa barani Afrika inayotoa huduma za kifedha zisizo za kibenki.

Kabla ya uzinduzi rasmi, SanlamAllianz tayari ilikua imeanza kugusa maisha ya watu kupitia shughuli mbalimbali za jamii. Ili kuongeza hamasa, kampuni hiyo kupitia wawakilishi wao waliofahamika kama ‘Men in Blue’ ilitoa msaada kwa Watanzania zaidi ya 145.

Pia, watanzania 40 walilipiwa gharama za huduma za afya. Vilevile, kampuni iliwalipia nauli abiria zaidi ya 75 waliokuwa wakisafiri katika maeneo ya Tandika na Mbagala. Hatua hizi zilikuwa sehemu ya shughuli za awali za kampuni katika kuunga mkono jamii kabla ya uzinduzi rasmi wa chapa mpya ya SanlamAllianz.

Hafla ya uzinduzi ilifanyika jijini Dar es salaam na kuhudhuriwa na wadau mbalimbali muhimu, ikiambatana na hafla ya chakula cha jioni iliyopambwa na mgeni rasmi, kamishna wa Bima kutoka Mamlaka ya Usimamizi wa Bima Tanzania (TIRA), Dkt. Baghayo Saqware . Uwepo wake uliashiria umuhimu wa ukuaji wa sekta ya bima nchini na mchango mkubwa ambao SanlamAllianz bima nchini na mchango mkubwa ambao SanlamAllianz inakusaidia katika kukuza soko la bima nchini Tanzania.

Kupitia kampuni zake mbili SanlamAllianz General Insurance Tanzania Ltd na SanlamAllianz Life Insurance Tanzania Ltd, kampuni imejipanga kutoa huduma bunifu na jumuishi za kifedha na bima, ikichanganya uzoefu wa kimataifa na uelewa wa ndani ya nchi ili kuwawezesha Watanzania kulinda maisha yao, biashara zao, na mustakabali wao wa kifedha.