May 16, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Sakata la Bandari laendelea kuwaibua wabunge,Musukuma asema wanaopinga hawana uelewa

Na Zena Mohamed,Timesmajiraonline,Dodoma.

SAKATA la makubaliano ya ushirikiano baina ya Serikali ya Tanzania na Dubai katika uendeshaji wa bandari nchini bado ni kizungumkuti na limeendelea kuwaibua wabunge wa Bunge la jamhuri ya muungano wa Tanzania kulizungumzia baada ya Jana Mbunge wa Jimbo la Mvumi kulizungumzia na kumataja Mbowe kupotosha umma leo Juni 9,2023 Mbunge wa Geita Vijijini Joseph Musukuma amezungumza na Vyombo vya habari jijini hapa na kusema kuwa yanayoendelea mitandaoni ni upotoshaji kuhusu mkataba huo.

Mbunge Musukuma ambaye pia ni mfanyabiashara amesema wanaopotosha na kupinga jambo hilo hawana uelewa na watu wenye chuki.

Ameeleza kuwa kabla ya Bandari ya Dar es salaam kwenda kwenye huo mpango wa Serikali ya awamu ya sita kumekuwa na kampuni iliyokuwa inaendesha bandari inaitwa Ticts imekuwepo kwa takribani miaka 30, tangu mwaka 2000 hadi 2016 Tanzania ilikuwa inalipwa kiasi cha Bilioni 7 peke yake, 2017 alipoingia awamu ya Tano ndo wakapanda kwenda kwenye bilioni 28, na kusema huwa Ticts hakuwekwa na Serikali ya awamu ya sita.

“Naweza kusema hii ni vita ya kiuchumu wale waliotolewa hawajaridhika, kwani Kampuni ya Ticts tangu imekuwepo imeleta mashine Saba pekee kwa kipindi chake cha Miaka 20 huku anayekuja (Dp world) analeta mashine zaidi ya hamsini katika kipindi cha Serikali ya awamu ya Tano Bunge lilipitisha Azimio la Bomba la Mafuta na Kodi zote za kusafirisha mafuta kwenye Bomba na kupata uwekezaji wa Trilioni 8.7 na hizo kelele mbona hazikuwepo?amehoji Musukuma.

“Tumwachie Rais atimize ndoto zake na naamini Taasisi ya Urais ina watu wengi, si kweli kama ambavyo watu wanazungumza mitandaoni wana research iliyofanyika, na sisi Wabunge baadhi tumekwenda kuona na kuona ni kuamini, na siyo kwamba wanaozungumza mitandaoni wana uwezo mkubwa sana ila hawajui mateso ya bandarini” amesema Musukuma.

Mbunge Musukuma amesema Bandari ni lango kuu la uchumi na kwa sasa Bandari ya Dar es salaam inatoa kontena 750, laki nane na nusu, mpaka laki Saba na hamsini kwa Mwaka ambapo ukienda Mombasa wako zaidi ya Milioni moja, Beila wako zaidi ya Laki mbili na hii yote ni mizigo ya Tanzania na iwapo bandari itaboreshwa itapunguza safari za watu kufuata mizigo katika sehemu za mbali.

“watanzania wasubiri tutakuja kuulizana tu Mungu atupe uhai, hawa wanaopiga kelele mimi naamini ni chuki tu kama tuna lengo zuri la kuisaidia nchi yetu huu ndo wakati mwafaka wa kutoka hatua tuliyonayo kwenda katika hatua nyingine”

Musukuma amesema kuwa Kampuni ya Ticts ilikaa miaka Saba akitumia miundombinu mibovu ya TPA na Hayati Magufuli alinunua Mashine Mbili pekee na sasa watu wanatoka kwenye Analogia kwenda Digitali na bado watu wanapiga kelele.

“ifikie kipindi lazima tubadilike, hivi nani anaweza kuja kusubiri Storage ya Kontena linakaa wiki mbili , ukienda Ocean Road unakuta Meli kama Kumi zimekaa kusubiri, milango imejaa, tunahitaji kuwa na akili za kufikiria”amesema.

Hata hivyo Musukuma amesema Uchumi wa Tanzania haumilikiwi na wenye degree na wanaosumbua mitandaoni bali unamilikiwa na wenye Elimu za kawaida.

“Hili suala inabidi tuwe makini sana kwa sababu sisi ndo tunapata adha, najua kuna maneno watu wameaminishwa kwamba Bandari inauzwa Miaka 100 mimi ninalo Azimio la Bunge hapa nalisoma leo siku ya Tatu sijaona sehemu iliyoandikwa Miaka 100, tena limeandikwa Kiswahili, nisije nikasema labda kizungu nitasumbuka,”amesema.