May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

RUWASA Ruvuma kukamilisha miradi 19 ya maji

Na Albano Midelo,TimesMajira online, Ruvuma
WAKALA wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) mkoani Ruvuma imedhamiria kukamilisha miradi ya maji 19 ifikapo Juni 30 mwaka huu.

Meneja wa RUWASA Mkoa wa Ruvuma Mhandisi Rebman Ganshonga akitoa maelezo kuhusu utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maji mkoani Ruvuma

Meneja wa RUWASA Mkoa wa Ruvuma,Mhandisi Rebman Ganshonga, amesema miradi hiyo ikikamilika asilimia 72 ya wananchi takribani milion 1.5 waishio vijijini watapata maji safi na salama.

Ilani ya Chama Tawala CCM inaelekeza kuwa ifikapo mwaka 2025 asimilia 85 ya wakazi wa maeneo ya vijijini na asilimia 95 kwa mijini wawe wanapata huduma ya maji safi na salama.

Ili kuhakikisha kuwa malengo hayo yanafikiwa Meneja RUWASA Mkoa wa Ruvuma amesema hivi sasa wanatekeleza miradi mbalimbali ilioanishwa kwenye bajeti ya mwaka 2020/2021.

Hata hivyo amesema kuna miradi mitano iliyochukua muda mrefu kukamilika katika Mkoa wa Ruvuma,hata hivyo amesema tangu RUWASA kuanzishwa miradi mitatu miongoni mwa hiyo imekamilika.

Meneja wa RUWASA Mkoa wa Ruvuma Mhandisi Rebman Ganshango akitoa maelezo kwa Mkuu wa Mkoa wa Ruvuma Christina Mndeme katikati alipokagua mradi wa maji Kata ya Lilambo wilayani Songea.

Ganshonga ameitaja miradi hiyo iliyokamilika kuwa ni Likuyusekamaganga, Mkongo na Matemanga na kwamba hivi sasa inatoa huduma kwa wananchi na kwamba miradi miwili iliyobaki anasema ipo kwenye hatua mbalimbali za utekelezaji.

“Mkoa wa Ruvuma ulikuwa na jumla ya miradi sita yenye changamoto, lakini tangu RUWASA ianze kazi miradi mitano imekamilika na mmoja uliobaki upo kwenye hatua za mwisho za utekelezaji’’,amesisitiza.

Meneja wa RUWASA Mkoa wa Ruvuma amesema Katika mwaka wa fedha utakaoanzia Julai mwaka huu wanatarajia kutekeleza zaidi ya miradi 28 kwa gharama ya zaidi ya shilingi bilioni 12 na kwamba watatumia mito na visima katika kutekeleza miradi hiyo kama mikakati ya muda mfupi.

Kuhusu mikakati ya muda mrefu Ganshonga amesema Wizara ya Maji inatarajia kujenga mradi mkubwa ambao utatumia maji ya Ziwa Nyasa na utahudumia maeneo mbalimbali ya mkoa wa Ruvuma na mikoa jirani ya Lindi na Mtwara ambayo pia inakabiliwa na changamoto.

Mkuu wa mkoa wa Ruvuma Christina Mndeme anaipongeza serikali kwa kutoa zaidi ya shilingi bilioni saba kwa ajili ya kuboresha miundombinu na upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama kwa miji ya Songea, Mbinga na Tunduru.

Amesema kupitia RUWASA na SOUWASA, kazi kubwa imefanyika ambapo serikali imetoa zaidi ya shilingi bilioni tano kati ya bilioni saba kwa ajili ya uwekezaji katika sekta ya maji ndani ya mkoa wa Ruvuma.