April 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Bucha ya nyama ya wanyama pori yazinduliwa Katavi

Na Israel Mwaisaka, TimesMajira,Online Katavi

SERIKALI ya Mkoa wa Katavi,leo imezindua rasmi bucha ya kuuza nyama ya wanyama pori ambapo imetangaza kuwa kilo mmoja ya nyama hiyo itakuwa ikiuzwa kwa bei ya sh. 8,000.

Mkuu wa Mkoa huo, Juma Homera amesema hatua hiyo imefanyika ikiwa pia ni kumuenzi Hayati Rais John Magufuli ambaye aliagiza kuanzishwa kwa bucha hizo hapa nchini ili kuwapa wananchi fursa ya kupata kitoweo hicho, sambamba na kupunguza vitendo vya ujangili.

Akizindua bucha hiyo, Homera amesema Hayati Magufuli alipokuwa mkoani Katavi ndipo alipotoa agizo la kuanzishwa kwa bucha hizo katika mikoa yenye hifadhi za taifa za wanyamapori, pamoja na mapori ya akiba kitendo kitakacho sababisha watu waliokuwa wakiingia ndani ya hifadhi na kufanya ujangili kupata kitoweo kuacha vitendo hivyo.

Aidha mkuu huyo wa Mkoa ametoa wito kwa wananchi wengine wenye nia ya kuanzisha bucha hizo kufuata utaratibu ili waweze kupata vibali vya kuanzisha bucha hizo ili wananchi wawe wanapata nyama za wanyama pori kirahisi na kuepuka kufanya ujangili.

Mkuu huyo wa Mkoa amesema kuwa katika kipindi hiki cha masika nyama katika bucha hiyo itakuwa ikipatikana mara tatu kwa wiki, lakini kipindi cha kiangazi itakuwepo kila siku kwani uwindaji utakuwa ukifanyika mara kwa mara.

Baada ya kuzindua bucha hiyo Serikali ya mkoa huo ilitumia fursa hiyo kuwafuturisha nyama hiyo ya pori baadhi ya wazee wa dini ya kiislaamu ambapo waliishukuru Serikali na kusema kuwa haijawahi kutokea katika mfungo wa mwezi mtukufu wa Ramadhani kufuturishwa kwa nyama za pori hii imekuwa ni mara ya kwanza kwao.

Kwa upande wake Meneja wa Pori la Akiba Rukwa (TAWA) Baraka Balagaye ametoa wito kwa yoyote ambaye anataka kufungua bucha ya nyama pori wao kama wasimamizi wa mapori ya akiba wapo tayari kutoa ushirikiano wa kutosha kufanikisha kufunguliwa mabucha ya kuuza nyama ya pori.