Judith Ferdinand,Dodoma
Wajumbe wa Bodi ya Mfuko wa Barabara(RFB), wametembelea na kukagua utekekalezaji wa mradi wa matengenezo ya barabara katika barabara ya Dodoma hadi Kitinku yenye urefu wa Kilomita 66.7.
Ambapo bodi hiyo imeainisha sehemu zingine za barabara hiyo zinazohitaji kufanyiwa matengenezo zaidi.
Ziara hiyo ya kutembelea mradi wa matengenezo ya barabara ya Dodoma hadi Kitinku, unaotekelezwa kwa fedha za Serikali kupitia Mfuko wa Barabara, imeongozwa na Mwenyekiti wa Bodi ya Mfuko wa Barabara Mhandisi Mussa Bally Natty.

Awali wajumbe hao, walikagua matengenezo mbalimbali ya miundombinu ya barabara ikiwemo ujenzi wa mtaro wenye urefu wa mita 450 pembezoni mwa barabara ya Dodoma hadi Kitinku, eneo la Kizota.
Mtaro huo umejengwa ili kuzuia uharibifu wa tabaka la barabara pamoja na kupunguza athari zitokanazo na mafuriko ya mvua kwa wakazi waishio maeneo ya jirani.
Aidha wajumbe hao pia, wamekagua matengenezo ya uwekaji wa tabaka jipya la barabara kwa kutumia zege katika eneo la Nala Mizani, kwenye barabara hiyo ya Dodoma hadi Kitinku, ambapo matengenezo hayo yanalenga kuimarisha na kupunguza athari za uharibifu wa barabara unaotokana na uzito wa magari makubwa yanayotumia Mizani ya Nala.
Vile vile Bodi hiyo imejionea ukarabati wa tabaka la jipya la barabara kwa kutumia lami (mita 150), kwa sehemu zilizokuwa zimeharibika na kusababisha usumbufu kwa watumiaji wa barabara ya Dodoma hadi Kitinku katika eneo la Bahi.

Kwa upande wake Kaimu Meneja wa Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS), Mkoa wa Dodoma Mhandisi Christina Nyamziga, amesema kuwa, utekelezaji wa mradi wa matengenezo ya barabara ya Dodoma hadi Kitinku yenye urefu wa Km 66.7), umegharimu kiasi cha milioni 911.
Mhandisi Nyamziga,amesema mpaka sasa utekekalezaji wa mradi huo umefikia hatua za mwisho na tayari upo katika hatua za maangalizi.
Hata hivyo Bodi ya Mfuko wa Barabara inaendelea na zoezi la ukaguzi wa kazi za matengenezo ya barabara katika Mikoa ya Singida, Manyara na Arusha, ili kujionea utekelezaji wa miradi hiyo inayofanywa kwa fedha za Serikali kupitia mfuko huo.



More Stories
Usajili wa Laini za Simu: Jilinde Dhidi ya Kutumiwa Vibaya kwa Utambulisho Wako
TTCL yaadhimisha siku ya Wanawake kwa kutoa msaada JKCI
Wananchi Dodoma washauri TBA kujenga nyumba za kupangisha watu binafsi