March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

RC Makalla:Uhusiano wa Dar,Hamburg wafanikisha uzinduzi kiwanda cha Mboji

Na Mwandishi wetu,timesmajira,Online

Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam, Amos Makalla,amezindua Kiwanda Cha Kuchakata taka na kuzigeuza kuwa Mbolea halisi Cha Mabwepande kilichojengwa kwa gharama ya Shilingi Bilioni 6 ikiwa ni ufadhili wa Serikali ya Ujerumani na Tanzania kupitia ushirikiano baina ya Jiji la Dar es salaam na Jiji la Hamburg.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, RC Makalla amesema Kiwanda hicho kimekuja wakati muafaka ambao Bei ya mbolea imepanda Kutokana na Vita inayoendelea baina ya Urusi na Ukraine na kutoa wito kwa Wananchi kununua mbolea hiyo.

Aidha RC Makalla amesema uwezo wa Mkoa huo ni kuzalisha zaidi ya Tani 23 za taka kwa siku hivyo kupatikana kwa Kiwanda hicho itasaidia kuwa na uhakika wa mahala pa kuzipeleka.

RC Makalla ametoa wito kwa Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni kusimamia Vizuri uendeshaji wa Kiwanda kwa kuhakikisha uzalishaji wa malighafi unakuwa wa kutosha.

Pamoja na hayo RC Makalla amesema kuwa siku ya kesho Julai Mosi Meya wa Jiji la Hamburg na Meya wa Jiji la Dar es salaam wanataraji kusaini mkataba wa mashirikiano katika kukabiliana na Changamoto ya mabadiliko ya tabia Nchi ambapo wamempongeza Rais Samia Suluhu Hassan kudumisha ushirikiano baina ya Tanzania na mataifa mbalimbali.

Uzinduzi wa Kiwanda hicho umeshuhudiwa pia na Balozi wa Ujerumani Nchini Tanzania na jopo la ujumbe wa wageni 46 kutoka Jiji la Hamburg nchini Ujerumani.