April 20, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Afisa wa Vijana wa Mkoa wa Dar es Salaam Masalida Zephania (aliyesimama) akiwasihi wahitimu wa chuo cha Amana vijana Centre hawapo pichani katika mahafali ya 9 kutumia taaluma zao vizuri katika kujipatia vipato endelevu. Kushoto kwake ni Mkurugenzi wa Amana vijana Cenre Philipo Ndokeji na Muhasibu wa chuo Magoye Luchagula wengine ni walimu wa chuo hicho. (Mpiga Picha Wetu)

RC Dar awaasa wahitimu Amana Vijana Centre

Na Bakari Lulela

WAHITIMU wa Chuo cha Amana Vijana Centre jijini Dar es Salaam wametakiwa kutumia taaluma walizozipata chuoni hapo kuwa nguzo ya kufungua milango ya fursa za ajira kwa kujipatia vipato endelevu.

Jumla ya wanafunzi waliohitimu chuoni hapo walikuwa 325 ambapo wasichana wakiwa idadi ya 205 huku wavulana 120 katika kozi tofauti.

Afisa wa Vijana wa Mkoa wa Dar es Salaam Masalida Zephania (aliyesimama) akiwasihi wahitimu wa chuo cha Amana vijana Centre hawapo pichani katika mahafali ya 9 kutumia taaluma zao vizuri katika kujipatia vipato endelevu .Kushoto ni Mkurugenzi wa Amana vijana Centre Philipo Ndokeji na Mhasibu wa chuo hicho Magoye Luchagula na wengine ni walimu wa chuo hicho. (Mpiga Picha Wetu)

Akizungumza Dar es Salaam wakati akimuwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam katika mahafali ya 9 ya chuo hicho Afisa vijana wa Mkoa wa Dar es Salaam Abubakar Kunenge, Masalida Zephania amesema elimu ni nguzo bora na ni msingi kwa mafanikio ya vijana wetu.

“Ipo haja kwa wazazi na walezi kuwapa miongozo sahihi vijana wao kujita katika kutafuta elimu kwenye vyuo mbalimbali vilivyoko hapa nchini ili kupata ujuzi utakuwa na manufaa kwao na Taifa kwa ujumla,” amesema Zephania.

Zephania amesema kuwa mafanikio hayaji hivi hivi bila kufanya jitihada, uvumilivu na kujituma hivyo aliwataka wahitimu hao kuwa na mazoea ya kuthubutu kwa makusudio ya kuanzisha viwanda vidogo vidogo.

Aidha afisa huyo alieleza Serikali imeweka mazingira mazuri kwa vijana wanaopata elimu ya vyuo vikuu kwa kuwapatiwa mikopo bila bugudha yeyote ili mradi wawe na sifa stahiki ya kuweza kupata huduma hiyo.

Hata hivyo kiongozi huyo alisema katika halmashauri zote nchini tumetenga kiasi cha asilimia 10 ya fedha kwa ajili ya makundi maalumu ambapo asilimia 4 kwa akinamama asilimia 4 kwa wajasiliamari na asilimia 2 kwa watu wenye ulemavu.

Kwa upande wake mkurugenzi wa chuo hicho Philipo Ndokeji amesema anawatakia kila heri wahitimu hao ila aliwataka wakumbuke nidhamu ni kitu cha msingi katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Amesema chuo kinatoa mafunzo ya kozi za kompyuta,Kiingereza,Hotel management, Mapambo na Saloon ambayo hutolewa bila gharama ,mbali na kutoa taaluma Amana Vijana Centre huwafundisha vijana namna ya kupambana na maisha.

Naye kijana aliyehitimu mafunzo ya kompyuta Salumu Zuberi amesema ujuzi alioupata katika chuo cha Amana itakuwa ni dira na chachu ya mafanikio huko waendako na kuwataka vijana wengine walioko mtaani kuchangamkia fursa hiyo .

Katika hafla hiyo walikuwepo maafisa kutoka Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) walishiriki kutoa elimu kwa wazazi na vijana kujiunga na huduma zao kwa hiari kwa manufaa ya baadaeni.