October 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Rasmi Yanga wamsimamisha kazi Wakili Patrick

Na MWandishi wetu, TimesMajira Online

KAMATI ya Utendaji ya klabu ya Yanga rasmi imetangaza kumsimamisha kazi Kaimu Katibu Mkuu wake ambaye pia ni Mkurugenzi wa Sheria na Wanachama, wakili Simon Patrick.

Minong’ono ya bosi huyo kutimuliwa Yanga ilianza kusikika toka wiki iliyopita lakini viongozi hawakuwa tayari kulitolea ufafanuzi suala hilo.

Lakini taarifa kutoka ndani ya klabu hiyo zinadai kuwa, kiongozi huyo anatajwa kuihujumu timu hiyo kwa kutoa siri na lizipeleka kwa wapinzani wao jambo ambalo linaweza kukwamisha mikakati yao ya kutwaa ubingwa wa msimu huu wa Ligi Kuu Tanzania Bara (VPL).

Pia inasemekana kuwa, kuanzia sasa majukumu ya Wakili Patrick yatakuwa chini ya Mwenyekiti wa klabu hiyo Dkt. Mshindo Msolla.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo na Mwenyekiti wa klabu hiyo, Dkt. Mshindo Msolla imeweka wazi kuwa wameamua kufikia maamuzi hayo baada ya kikao cha dharura cha Kamati ya Utendaji kilichokaa jana Novemba 17, 2020 ambacho kilifanyika maalum kwa ajili ya kusikiliza shutuma ambazo amehusishwa nazo.

Kwa dhumuni la kuhakikisha haki inatendeka, Kamati ya Utendaji itateua Kamati Huru kuchunguza swala hili na kutoa maamuzi yenye tija kwa pande zote.

Hivyo, Kamati ya Utendaji itaisubiri Kamati Huru kukamilisha uchunguzi wake na kutoa ripoti juu ya tuhuma hizi.