May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Ramadhani Brothers watembelea Makao Makuu ya TANAPA

Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online

WASHINDI wa tuzo za American Got Talent, ambao ni wasanii katika mchezo wa sarakasi, Ramadhani Brothers wametembelea Ofisi za Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Mei 6 mwaka huu kwa ajili ya kujionea mambo mbalimbali yanayofanywa na shirika hilo.

Mara baada ya kufika katika ofisi za Shirika hilo walikaribishwa na Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi, Angela Nyaki baada ya kukamilisha safari ya kupanda mlima mrefu zaidi barani Afika, Mlima Kilimanjaro kwa kufika kileleni.

Kamishna Nyaki aliwapokea kwa kuwakaribisha Shirika la Hifadhi za Taifa ambapo alitumia muda huo kuwapa zawadi mbalimbali.

Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi ambaye pia Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Kilimanjaro, Angela Nyaki(katikati) akimkabidhi zawadi mmoja wa Ramadhani Brothers (kulia), walipotembelea Ofisi za Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Mei 6 mwaka huu kwa ajili ya kujionea mambo mbalimbali yanayofanywa na shirika hilo. Picha na TANAPA

Wasanii hao walitembelea ofisi hizo walipokuwa wakielekea Hifadhi ya Taifa Serengeti wakiwa katika zoezi maalumu la kuhamasisha kampeni ya VOTE NOW.

Kampeni hiyo mahususi kwa ajili ya kupigia kura hifadhi ya Taifa Serengeti na Mlima Kilimanjaro zinazowania tuzo za ‘World Travel Awards’, katika kipengele cha Africa’s leading national park wakati Kilimanjaro ikiwania tuzo katika kipengele cha Africa’s leading tourist attraction.

Baada ya kufika katika Ofisi za TANAPA, Vijana hao walitembelea Hifadhi bora barani Afrika, Hifadhi ya Taifa Serengeti ambayo imeshinda tuzo ya kuwa hifadhi bora Afrika mara tano (5) mfululizo.

Mara baada ya kufika Serengeti, walifurahi sana na kuahidi kuwa watakuwa mabalozi wa kutangaza vivutio vya Tanzania pindi watakapokuwepo nje ya mipaka ya Tanzania.

“Tumefurahia sana kutembelea Hifadhi za Taifa, tunawapongeza sana kwa kazi kubwa mnayoifanya TANAPA, kulinda maliasili za Taifa letu nasi tutakuwa Mabalozi kutangaza vivutio vyetu tuwapo nje ya mipaka ya Tanzania,” wamesema Ramadhan Brothers.