April 26, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Rais Samia Kuwa mgeni rasmi siku ya ukimwi duniani

Na Esther Macha,Timesmajira,Online, mbeya

MKOA wa Mbeya unakadiliwa kuwa na  watu 142,784 ambao  wanaishi na maambukizi ya virusi vya ukimwi na kwamba  hadi kufikia mwezi  juni mwaka  huu jumla ya watu 116,610 sawa na na asilimia 82 wote wanatambua  hali zao.

Hayo yamesemwa  leo na Mkuu wa Mkoa wa Mbeya ,Juma Homera wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusiana na maadhimisho ya siku ya ukimwi duniani ambayo kitaifa inafanyika Mkoani Mbeya na Rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika maadhimisho hayo.

Homera amesema kuwa kati ya hao watu 115,942 ambayo ni sawa na asilimia 99.3 wapo kwenye huduma za tiba na matumizi ya dawa na asilimia 96.7 waliopo kwenye tiba.

Aidha Mkuu huyo wa Mkoa amesema kuwa utafiti wa kiashiria wa mwa mwaka 2016-2017 unaonyesha kuwa  kiwango cha maambukizi ya virusi vya ukimwi ni 9.3 kwa watu wenye umri wa miaka 15 mpaka 49  tofauti na takwimu za mwaka 2011/2012 ambapo kiwango cha maambukizi ilikuwa asilimia 9.0.

“Ukilinganisha na kiwango cha maambukizi kitaifa ambayo ni asilimia 4.7 hivyo tumevuka lengo la kitaifa, tunahitaji ushirikiano wa wadau mbalimbali ili kuhakikisha tunashusha kiwango hicho,”amesema Homera.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Kuthibiti Ukimwi Tanzania (TACAIDS), Dkt. Leonard Maboko alisema kuwa  katika maadhimisho hayo kutakuwa na shughuli mbalimbali ambazo zitakuwa zikiendelea kwenye maonyesho hayo.

Amesema kutakuwa na upimaji wa hiyari wa VVU na magonjwa mengine ambapo aliwataka wananchi wa Mkoa wa Mbeya na mikoa jirani kuchangamkia fursa hiyo.

Dkt. Maboko amesema wamewaalika wadau mbalimbali wa mapambano dhidi ya Ukimwi ambao wamethibitisha kushiriki maadhimisho hayo ikiwemo kwenye matembezi ya hisani.

Kwa upande wake Mwakilishi wa Baraza la Taifa la watu wanaoishi na Virusi vya Ukimwi, Joceline Mtono ameishukuru Serikali kwa kuendelea kuwahudumia ikiwa ni pamoja na kuwapatia bure dawa za kufubaza VVU.