May 19, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Rais Samia ataka uvuvi haramu ukomeshwe

Judith Ferdinand,Timesmajira Online,Mwanza

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassana ameitaka Wizara ya Mifugo na Uvuvi kushirikiana na seketarieti ya Mikoa na Halmashaur kudhibiti na kutokomeza vitendo vya uvuvi haramu huku akiitaka iwachukulie hatua kali za kisheria wavuvi wanao kiuka taratibu za uvuvi salama.

Rais Samia ameyasema hayo Januari 30,mwaka huu katika hafla ya uzinduzi na ugawaji wa boti za kisasa za uvuvi na vizimba vya kufugia samaki kwa wavuvi wa Kanda ya Ziwa iliofanyika uwanja wa Nyamagana jijini Mwanza mwenye kauli mbiu isemayo”Uchumi wa buluu ni fursa muhimu kwa wananchi”.

Ambapo jumla ya boti 160 za uvuvi za kisasa zimezundiliwa kati ya hizo 55 ni kwa Kanda ya Ziwa kwa wanufaika 989 pamoja na vizimba 222 kwa wanufaika 1,213 katika mikoa ya Kanda ya Ziwa ikiwemo Mwanza,Kagera,Geita,Simiyu na Mara.

Ameeleza kuwa shughuli za uvuvi ziendeshwe kwa kuzingatia sheria,kanuni na taratibu kwa kudhibiti na kukomesha vitendo vya uvuvi haramu huku wakiwachukulia hatua za kisheria watakaoendekeza vitendo hivyo.

“Uchomaji wa nyavu kwa lengo la kukabiliana na uvuvi usio takiwa unarudisha nyuma maendeleo ya uvuvi na kugombanisha serikali na wavuvi wanaochomewa nyavu zao,utoaji wa vifaa vya kisasa nina hakika nyavu zilizotolewa leo si nyavu za makokolo ambazo zinakatazwa ni nyavu njema kwaio niombe Wizara muongeze kasi katika kusambaza nyavu zile kwa njia ya mikopo ili wavuvi wasitumie nyavu zinazokatazwa,”ameeleza Raisa Samia na kuongeza kuwa

“Jambo la pili ni elimu kwa wavuvi wetu muwe karibu sana na kama mtaturidhusha mkaunda Wakala wa Uvuvi basi Wakala wa Uvuvi utoe elimu ya kutosha kwamba uvuvi wanaofanya wa makokolo una maliza rasilimali zetu na vifaa tunavyo vitoa mkiendelea na mkiwa mnafanya na makokolo mnaenda kumaliza rasilimali ile na vifaa vya kisasa havitapata mazao ya kuvua,”.

Pia ameeleza kuwa kundi la vijana na wanawake linaongoza kushirika katika ajira zisizo rasmi hivyo serikali inarasimisha shughuli zao kwa kuwawezesha kupata zana na nyenzo za kisasa ili kutoka katika kujikimu hadi kufanya biasahara ambapo sekta ya uvuvi inaweza kutoa wafanyabiashara wakubwa.

Sanjari na hayo Rais Samia ameeleza kuwa serikali imejipanga kukuza sekta ya uvuvi kupitia miradi mbalimbali ikiwemo ununuzi wa meli wa meli za kisasa za uvuvi katika bahari kuu,ujenzi wa bandari za uvuvi Kilwa Masoko mkoani Lindi na Bagamoyo ili kuongeza pato la taifa.

“ Sekta ya uvuvi ina mchango mdogo katika pato la taifa la asilimia 1.8 ukilinganisha na rasilimali ziliopo hivyo serikali inafanya jitihada kuinua sekta hiyo nchini kwa kuimarisha utendaji wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi ili iendane na dhamira ya mageuzi iliokusudiwa,”.

Kwa upande wake Waziri wa Mifugo na Uvuvi Abdallah Ulega ameeleza kuwa kwa mwaka huu wa 2024-2025 kutokana na mahitaji makubwa ya Watanzania ya zana hizo za kisasa wamedhamiria waweke boti zisizopungua 500 ziende nchini kote.

Pia ameeleza kuwa vizimba,boti na vifaranga vya samaki alivyotoa Rais Samia vyote vimekatiwa bima na Shirika la Taifa ya Bima(NIC), ambapo katika mwaka wa fedha 2022/23 kiasi cha bilioni 60 zilitolewa kwa miradi ya maendeleo ikiwemo ujenzi wa mialo na masoko ya samaki ambapo kila senti katika mwaka 2023/24 itafanya kazi ya kuwanufaisha Watanzania.

Ulega ameleza kuwa Wizara ina mkakati wa kuwa na chombo kimoja ambacho kitasimamia sekta ya uvuvi itakayoongeza mchango wa pato la taifa toKa asilimia 1.8 hadi asilimia 10 mwaka 2036-2037 na kuongeza uzalishaji wa samaki toka tani laki tano mwaka 2023 hadi tani laki saba.

“Boti 160 za kisasa za uvuvi zimezinduliwa kwa wanufaika 989 kati ya hizo 55 ni kwa Kanda ya Ziwa pamoja na vizimba 222 vya kufugia samaki vitakavyonufaisha 1,213 katika mikoa ya Mwanza,Mara,Kagera,Simiyu na Geita,”alisema Ulega.

Akitoa salamu za Mkoa Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Amos Makala, ameeleza kuwa uvuvi haramu umeathiri kwa kiasi kikubwa sekta ya uvuvi hivyo yeye na Wakuu wenzake wa mikoa ya Kanda watahakikisha wanaweka mikakati ya kuwa na uvuvi endelevu katika Ziwa Victoria.

“Utafiti uliofanyika mwaka 2018-2022, ulibaini wingi wa samaki ulipungua kwa asilimia 30 na kulikuwa na viwanda vya kuchakata samaki 15 ila sasa 8 ndio vinafanya kazi vimeathiriwa na uvuvi haramu kama Mkoa tumechukua hatua katika uvuvi haramu na kufanya uvuvi endelevu,”Makala.

Mmoja wa wanufaika wa mradi huo Pius Mtenya ameiomba serikali kuwezesha miundombinu katika maeneo ya miradi yao ikiwemo barabara,kujengwe viwanda cha barafu pamoja na vya kuzalisha chakula cha samaki pia iwahakikishie upatikanaji wa mbegu bora za vifaranga wa samaki.