May 17, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Rais Samia apongezwa kwa miradi ya maji Biharamulo

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online

MKUU wa Wilaya ya Biharamulo, mkoani Kagera, SACP Advera Bulimba, amepongeza juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kutokana na kupeleka fedha zilizofanikisha wananchi 314,212 kupata huduma ya maji safi na salama wilayani humo.

Akizungumza mjini Biharamulo, SACP Advera alisema kwa kipindi cha mwaka 2021 hadi 2024, Rais Dkt. Samia amepeleka wilayani Biharamulo sh. 8,800,811, 050.86 zilizotumika kutekeleza miradi ya maji kupitia Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA).

Alisema fedha hizo zimesaidia kuongeza hali ya upatikanaji huduma ya maji kutoka asilimia 52 mwaka 2020 hadi kufikia asilimia 68.5 Desemba, 2023.

“Hadi sasa RUWASA imeweza kufikia vijiji 34 kati ya vijiji 64 ambapo jumla ya wananchi 314,212 wanapata huduma ya maji safi na salama, kwa hili tunamshukuru sana Rais Dk. Samia kwa kutuletea fedha ambazo zimefanikisha utekelezaji wa miradi ya maji wilayani Biharamulo,” alisema.

Kwa mujibu wa SACP Advera, RUWASA wilayani humo inahudumia jumla ya kata 14 kati ya 17, ambazo ni Ruziba, Katahoka, Nyamahanga, Runazi, Kabindi, Nyamigongo, Nyabusozi, Nemba, Lusahunga, Kaniha, Nyantakara, Nyanza, Nyarubungo na Kalenge.

Mkuu huyo wa wilaya alitaja baadhi ya vijiji na idadi ya miradi ya utafiti na uchimbaji visima virefu iliyokamilika ni Migango (7), Kaniha (2), Kagoma, Lusahunga, Busiri, Ntumagu na Songambele (11), Kisenga, Nemba, Kaluguyu na Kalenge (9).

Vijiji vingine ni Nyamigongo, Rukirilwengoma, Kaperanono, Nyamtongo na Nyakahura (7) ni Kabindi, Chebitoke, Rukora, Kikomakoma (1), Runazi (1), Nyantakara (1), Kabukome (1), Lusahunga na Nyambale (1).

SACP Advera aliongeza wilaya hiyo mwaka 2023/24 ilitengewa sh. 6,741, 922, 263 za maendeleo kutokana na vyanzo vya fedha ambavyo ni PforR, Mfuko wa Maji wa NWF na ruzuku ya maendeleo (GOT).

“Fedha hizo zitatumika kutekeleza miradi ya maji vijiji vya Kasato, Kitwechemgogo, Ruziba, Kalebezo, Rukililwengoma, Katoke, Nyarubungo, Nyamahanga, Ntungamo, Lusahunga- Nyagurube, Runazi-Mwembeni, Kibindi na Nyakahura,” alisema.

Mkuu huyo wa wilaya alibainisha baadhi ya miradi hiyo ipo katika hatua za manunuzi, usanifu na kutafuta chanzo.