Na Mwandishi wetu, Timesmajira
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, amewaongoza Viongozi mbalimbali na mamia ya Wananchi katika maziko ya Marehemu Charles Martin Hilary, aliyekuwa Msemaji Mkuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Mkurugenzi wa Idara ya Mawasiliano Ikulu.
Mapema, Rais Dkt. Mwinyi aliwaongoza Viongozi na Wananchi katika Ibada ya kuuaga mwili wa marehemu, iliyofanyika katika Viwanja vya Mapinduzi Square, Michenzani – Wilaya ya Mjini.

Akizungumza katika hafla hiyo, Rais Mwinyi amemuelezea Marehemu Charles Hilary kuwa ni mchapakazi, mcheshi, mtu wa watu, na mzalendo wa kweli aliyeipenda nchi yake kwa dhati.
Dkt. Mwinyi amewanasihi Watendaji wa Serikali kuwa na utamaduni wa kuwasifu na kuthamini watendaji wazuri wakiwa hai, badala ya kusubiri mpaka wafariki dunia.
Aidha, Rais Dkt. Mwinyi amesisitiza kuwa Taifa lina wajibu wa kuendelea kumuenzi Marehemu Charles Hilary kwa utendaji wake uliotukuka katika dhamana alizomkabidhi wakati wa uhai wake.

Vilevile, Rais Dkt. Mwinyi ameifariji familia ya Marehemu Charles Hilary, akiwemo mjane wa marehemu, Bi. Sarah Mwakanjuki, na kuwataka wawe na subira na moyo wa uvumilivu katika kipindi hiki kigumu cha msiba.
Misa ya kumuombea marehemu imefanyika katika Kanisa Kuu la Anglikana, Mkunazini.
Akitoa salamu za familia, Mtoto wa marehemu, Faith Charles Hilary, ameishukuru Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa heshima kubwa aliyopewa Marehemu Charles Hilary wakati wa uhai wake, kwa kumuamini katika nyadhifa muhimu Serikalinina kumuaga kwa heshima baada ya kifo chake.
Marehemu Charles Hilary alifariki dunia tarehe 11 Mei 2025 akiwa njiani kupelekwa Hospitali ya Mlonganzila, Dar es Salaam kwa ajili ya matibabu. Ameacha mjane na watoto wawili.
More Stories
Lulida ataka viwanda vilivyofungwa vifufuliweÂ
WMA yahakiki vipimo asilimia 99 ya lengo
Kapinga :Serikali inaendelea kutekeleza miradi ya umeme kwenye maeneo ya kimkakati