October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli. Picha ya Maktaba

Rais Magufuli ateua DC mpya Ilala,viongozi wengine

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dkt.John Pombe Magufuli amemteua, Ng’wilabuzu Ndatwa Ludigija kuwa Mkuu wa Wilaya ya Ilala mkoani Dar es Salaam.

Kabla ya uteuzi huo, Ludigija alikuwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Kigamboni mkoani Dar es Salaam na anachukua nafasi ya Mussa Ramadhan Chogelo ambaye amepangiwa kazi maalum katika Ofisi ya Rais.

Kufuatia uteuzi huo,Rais Magufuli amemhamisha kituo cha kazi Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mpimbwe mkoani Katavi, Erasto Nehemia Kiwale ambaye anakwenda kuwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Kigamboni mkoani Dar es Salaam.

Kiwale anachukua nafasi ya Ng’wilabuzu Ndatwa Ludigija ambaye ameteuliwa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Ilala.

Wakati huo huo,Rais Magufuli amemteua Catherine Michael Mashalla kuwa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mpimbwe mkoani Katavi.

Kabla ya uteuzi huo,Mashalla alikuwa Afisa Elimu wa Manispaa ya Kigamboni mkoani Dar es Salaam na anachukua nafasi ya Erasto Nehemia Kiwale ambaye amehamishwa kituo cha kazi na kuwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Kigamboni.

Kwa mujibu wa taarifa ya Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Gerson Msigwa, uteuzi na uhamisho wa viongozi hao unaanza leo.