May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

PURA kuendelea na udhibiti wa shughuli za uzalishaji gesi

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

MAMLAKA ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) itaendelea na usimamizi na udhibiti wa shughuli za uzalishaji na utafutaji gesi asilia, ili kuhakikisha shughuli hizo zinafanywa kwa mujibu wa sheria.

Hayo yamebainishwa Jana Julai 5, 2023 na Mkurugenzi Mkuu wa PURA Mhandisi Charles Sangweni akizungumza na waandishi wa habari kwenye banda la PURA lililopo katika viwanja vya Sabasaba jijini Dar es Salaam.

Amesema PURA itatumia Maonesho ya 47 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam kueleza Miradi wananchi Miradi wanayosimamia na tafiti walizofanya kwenye mafuta na gesi asilia.

Mhandisi Sangweni ametaja miongoni mwa Miradi hiyo kuwa na Mradi wa kubadili gesi waliyogundua katika Bahari kuu na kuweka kwenye hali ya kimiminika.

“Sisi kwenye tafiti tulianza tangu miaka 50 iliyopita na tumegundua gesi,” amesema Mhandisi Sangweni na kuongeza,

“Gesi hii ni chanzo cha Nishati nchini na hadi sasa tumechimba visima 96 vya gesi na Kati ya hivyo 44 tulivikuta na gesi na vingine vilivyobaki havikuwa na gesi,”.

Mhandisi Sangweni ameelendelea kueleza kwamba gesi tuliyonayo nchini inazalishwa kutoka Songosongo, Monazibey na Kwara na imekuwa ikitumika katika kuzalisha umeme wa viwandani, majumbani na kadhalika.

“Asilimia 60 ya umeme tunaotumia nchini inatokana na gesi,” amesisitiza Mhandisi Sangweni.

Aidha amebainisha kuwa katika tafiti zao hadi sasa wamegundua futi za ujazo Trilioni 57.5 za gesi.Amesema kuwa kama PURA ndiyo Mamlaka ambayo inamshauri Waziri wa Nishati katika Uwekezaji wa nisahti ya mafuta na gesi katika Mkondo wa Juu.

Vile vile wanatoa ushauri kwa Waziri wa Nishati kutoa Leseni ya uchimbaji wa gesi.