October 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

PST yaweka mkakati kupeleka ngumi kimataifa

Na Yusuph Digossi, TimesMajira Online

VIONGOZI wa Shirikisho la Ngumi za Kulipwa nchini (PST) wameahidi kufanya mambo makubwa zaidi yatakayoufikisha mbali na kuutangaza kimataifa zaidi mchezo wa ngumi ambao kwa sasa unarudi kwa kasi kubwa.

Ahadi hiyo umetolewa na Katibu Mkuu wa Shirikisho hilo, Anthony Rutta mara baada ya kumalizika kwa mapambano ya wazi wa Kimataifa ‘Open Air International Boxing’ yatakayofanyika mwishoni mwa wiki katika Uwanja wa Mabembea uliopo Keko Magurumbasi.

Katika mapambano hayo, mabondia wa Uingereza walishindwa kutamba kwa mabondia wa Tanzania baada ya Jonh Brenannern akipingwa TKO ya raundi ya nne na Issa Mbwana katika pambano lisilo la ubingwa la raundi nane uzito wa kilogramu 69.85 Super Welterweight

Mtanzania Innocent Evarist na Muingereza Prince Patel wametoka sare na kupelekea mkanda waliokuwa wakigombea wa ‘WBO Global & Africa’ katika pambano la raundi 12 uzito wa kilogramu 52.16 Super Flyweight kubaki mezani.

Mwanadada Halima Vunjabei alimpiga mpinzani wake Maimuna Hashim TKO ya raundi ya pili wakati Sarai Amabo akishindwa kutamba mbele ya Ali Bakari aliyempiga kwa pointi.

Akizungumza na Mtandao huu, Rutta amesema kuwa, baada ya mapambano hayo ya wazi kufana huenda wakaja na kitu cha tofauti ambacho kitaurusha haraka zaidi mchezo wa ngumi mahali panapostahili.

Amesema wao kama Shirikisho ambalo limepeleka mabondia wengi zaidi katika mapambano ya nje, watahakikisha sasa wanaweka nguvu kubwa zaidi kuwaleta mabondia wa nje hapa nchini.

Pia watahakikisha wanajipanga zaidi katika maandalizi ili mataifa mengine hasa makubwa kuona haja ya kuja hapa nchini kwa ajili ya mapambano yako ukizingatia mipaka ya nchi nyingi bado imefungwa kutojana na janga la ugonjwa wa Covid-19.

“Tumeshaanza mikakati ya kujipanga kimataifa zaidi kwani tunahitaji kujijengea heshima kubwa Afrika na duniani, kama tumeanza kuleta mabondia kutoka Uingereza basi tunaamini itafika siku hata kina Anthony Joshua watakuja kufanyia mapambano yao hapa nchini kikubwa ni kujipanga na kutumia fursa zulizopo,” amesema Rutta.

Hata hivyo aliiomba Serikali kupitia Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo kuona haja pia ya kutenga fungu maalum kwa ajili ya mchezo wa ngumi ambao ni mchezo wa kwanza kuiletea nchi medali katika michuano ya Jumuiya ya Madola baada tu ya kupata uhuru.

Amesema, Katika takwimu za kimichezo hapa nchini, mabondia wengi wameitangaza nchi baada ya kutwaa mikanda mbalimbali yaAnthony Joshu kimataifa kuliko michezo mingine ikiwemo soka na riadha lakini hawaelewi kwanini umekuwa ukiwekwa nyuma.

“Ngumi tupo hatua 10 mbele zaidi ya michezo mingine kwani ni mchezo wa kwanza baada ya uhuru kuiletea nchi medali hivyo tunaiomba sana Wizara husika kuweka kuwa mamcho zaidi na kuweka jitihada zaidi katika mchezo huu kwani mikakati yetu ni kuifanya Tanzania kuwa bora zaidi Afrika na hata Duniani,” amesema Rutta.