*Ni zile zinazokusanya na kuchakata taarifa binafsi
*Yatoa muda wa mwisho usajili Aprili 30,2025
Judith Ferdinand, Timesmajira Online, Mwanza
Imeelezwa kuwa taasisi 2000 zinazohusika na ukusanyaji na uchakataji wa taarifa binafsi kati ya 140,000 nchini,zimejisajili kwenye Tume ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi(PDPC).Huku Mkoa wa Mwanza ukiwa ni moja ya Mikoa ambayo usajili wake upo chini ukiwa na taasisi 20 tu zilizojisajili mpaka sasa.
Kutoka na zoezi hilo kuwa na kasi ndogo,PDPC imetoa wito kwa taasisi zinazohusika na ukusanyaji na uchakataji wa taarifa binafsi, kujisajili kwenye Tume hiyo, kuzingatia sheria ikiwa ni pamoja na maandalizi muhimu ya kazi wanazofanya na kuhakikisha wanafahamu wapi panaweza kuwa na mwanya taarifa hizo kutumika vibaya.
Hayo yameelezwa Machi 22,2025 na Mkurugenzi Mkuu wa PDPC,Dkt.Emmanuel Mkilia,wakati akifunga warsha ya siku moja ya kuwajengea uelewa waandishi wa habari wa Mkoa wa Mwanza juu ya dhana mzima ya ulinzi wa taarifa binafsi,iliofanyika mkoani hapa,ambapo amesema baada ya Rais Samia Suluhu Hassan,kuzindua Tume hiyo,aliitaka kuhakikisha taasisi nyingi zinazokusanya na kuchakata taarifa binafsi zisajiliwe.
Mkilia, amesema wakusanyaji na wachakataji wa taarifa binafsi kujisajili kwao ni kuonesha msimamo na uimara wa kuhakikisha kuwa taarifa zile zitatumika kwa ajili ya matumizi kusudiwa na si vinginevyo.
“Wakuu wa taasisi zote za Serikali na Binafsi, kuhakikisha taasisi zao zimejisajili,ambapo zoezi la usajili limesogezwa.mpaka Aprili 30,2025 kwani awali lilikuwa likamilike Desemba 30,2024, na baada ya muda kupita wahusika watakuwa wanatenda kosa.Taasisi kubwa ni pamoja na za kifedha,kampuni za simu,kilimo,ufugaji wa samaki,usafiri na usafirishaji huku taasisi ndogo ni pamoja na nyumba za kulala wageni huko pote watu wanajaza taarifa binafsi,”.
Pia amesema,taasisi hizo kujisajili PDPC, itawezesha utaratibu wa mifumo yote ya Serikali na binafsi kusomana pamoja na Tume kusimamia jukumu waliopewa kisheria la kuhakikisha kwamba taarifa binafsi zinatumiwa kwa utashi na makundi kusudiwa na yanazingatia usalama.
Hata hivyo,amesema,mifumo ikisomana mtu atahudumiwa kutokana na utambulisho wake na kila mwananchi atakuwa na uwezo wa kujua taarifa zake zimetumika wapi kupitia Jamii Portal,ambayo inamruhusu kila mtu kuangalia taarifa zake zilitumika wapi na kwanini na je aliridhia au aku ridhia na kama taarifa zilitumika sehemu ambapo akurudhia ataiona Tume.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Usajili na Uzingatiaji kutoka PDPC, Mhandisi Stephen Wangwe,amesema taasisi hizo zinaweza kujisajili kwa njia mtandao,na mpaka sasa wameisha pokea malalamiko takribani 60 kati yao mengi yenye hali ya udhalilishaji.
“Mwananchi anahitaji kukopa kupitia wakopeshaji wa mitandaoni wa “apps”ambazo lazima upite hatua fulani ili iweze kupata huduma,katika hatua anazopita kuna sehemu mtumiaji anaulizwa unaturuhusu tumtumie orodha yako ya namba zilizopo kwenye simu yako”phone book”,wengi wamekuwa wakitiki sasa wakati wa malipo mtoa huduma anapeleka ujumbe wa kumdhalilisha yule mtu kwenye orodha ile.Tumeshirikiana na Benki Kuu ya Tanzania(BOT),Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania(TCRA) na vyombo vya ulinzi na usalama kuzifutia usajili taasisi zote zinazofanywa huduma hizo na tunatoa wito kwa watu kuwa makini na kile ambacho tunaomba,”.
Naye Mkuu wa Uhusiano na Mawasiliano kwa Umma wa PDPC, Innocent Mungy,amesema ulinzi wa taarifa binafsi ni muhimu katika uchumi wa kidigitali,kwani katika uchumi huo inahitajika imani kuweza kufanya biashara kwa njia ya mtandao.
“Mfano kuuza kwa bidhaa kwa kutumia mitandao,kufanya shughuli za kibenki(fedha), kupitia mitandao,kunapokuwa na ulinzi wa taarifa binafsi watu wanaingia kwenye biashara ya mtandao kwa sababu wanaimani kwamba taarifa zao zipo salama, na wanaweza kutumia kadi zao za benki na kufanya miamala bila ya wasiwasi,” amesema Mungy.
Mungy,amesema suala jingine la ulinzi wa taarifa binafsi ni kutengeneza fursa za kiuchumi kwa njia ya kidigitali ambazo zamani ilikuwa lazima mtu aende mahali kufanya biashara au kununua bidhaa.
“Lakini sasa hivi unatumia mitandao ya kijamii mtu anaweza akaagiza bidhaa siyo tu hapa nchini bali nje ya nchi na bidhaa ikamfikia mahali alipo, pia kuwezesha malipo mbalimbali ambayo yanafanyika katika uchumi wa kidigitali.Mtu anapokuwa na uhakika wa huduma zinazotolewa na taarifa zao kuwa salama ni rahisi kufanya uhamishaji wa fedha na kukuza uchumi wa nchi kupitia kidigitali,”.
More Stories
Msajili Hazina: Tuyaishi mafunzo ya mwezi mtukufu wa Ramadhani
TASHICO ya pokea kontena tano za samani kwa ajili ya MV.Mwanza
EWURA, ERB kushirikiana kuboresha huduma za nishati