October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akiweka udongo kwenye mti wa kumbukumbu alioupanda wakati wa uzinduzi wa chuo cha Ufundi Stadi Nyamidaho mkoani Kigoma.

Ndalichako azindua Chuo cha Ufundi Stadi Kigoma

Na Joyce Kasiki, TimesMajira Online

WAZIRI wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako amezindua Chuo cha Ufundi Stadi Nyamidaho kilichopo Wilaya ya Kasulu Mkoani Kigoma huku akisema kuanzishwa kwa chuo hicho ni mwendelezo wa utekelezaji wa azma ya Serikali ya Awamu ya Tano ya kujenga vyuo hivyo katika kila wilaya nchini.

Moja ya jengo lililojengwa katika chuo kipya cha Ufundi Stadi Nyamidaho mkoani Kigoma kilichozinduliwa na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako

Akizungumza katika hafla ya uzinduzi wa chuo hicho, Profesa Ndalichako amesema lengo la serikali ni kuhakikisha  huduma hiyo ya vyuo vya ufundi stadi inakuwa  karibu na wananchi na kuwawezesha kupata ujuzi wa aina mbalimbali na kujikwamua katika umasikini wa kipato.

Ndalichako amesema Chuo cha Nyamidaho kimetokana na majengo yaliyokuwa yakitumiwa na Taasisi ya World Vision ambapo Serikali imekarabati majengo yaliyokuwepo na kujenga mengine mapya.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akijaribu moja ya mtambo wa kisasa wa kufyatulia matofali unaotumika kufundishia katika chuo cha ufundi stadi Nyamidaho mkoani Kigoma.

Kwa mujibu wa Waziri Ndalichako jumla ya shilingi milioni 534 zilitolewa kwa ajili ya kazi hiyo na kwamba zimetumika milioni 477 hadi ukamilishaji. Aidha ameridhia ombi la kiasi kilichobaki kutumika kuanzisha ujenzi wa bweni la wanafunzi wa kiume.

Ndalichako amesema, katika mwaka 2019/20 vyuo 10 vya halmashauri za wilaya vimejengwa na kuanza kutoa mafunzo.

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Kigoma Brigedia Jenerali Emmanuel Maganga ameishukuru Wizara ya Elimu kwa kukamilisha ujenzi wa chuo hicho na amewataka wakazi wa Kijiji cha Nyamidaho kuhakikisha vijana wao hasa wa kike wanajiunga na chuo hicho.

Naye Mwenyekiti wa Bodi ya VETA, Peter Maduki ameishukuru serikali kwa kuendelea kuimarisha elimu ya ufundi nchini huku akisema kuwa Chuo hicho kipya kina wanafunzi takriban 70.

Maduki ametumia fursa hiyo kuuagiza uongozi wa VETA kutoa bure mafunzo ya kozi ya uwashi kwa wanafunzi wanaotoka Nyamidaho.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Profesa Joyce Ndalichako akiangalja baadhi ya vifaa vya kisasa vya ujenzi vinavyotumika kufundishia katika chuo kipya cha VETA Nyamidaho wakati wa uzinduzi wa chuo hicho