April 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

NBS: Rais Samia ameendelea kuiletea sifa Tanzania kimataifa

Na Zena Mohamed, TimesmajiraOnline, Dodoma

OFISI ya Taifa ya Takwimu (NBS) imeanika mafanikio ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, ambapo amefanikisha kupunguza vifo vinavyotokana na uzazi na pia kwa watoto chini ya miaka mitano na kuendelea kuweka rekodi na kuiletea sifa nchi kimataifa.

Hiyo ni kutokana na tatifi zilizofanywa na NBS ikiwemo utafiti wa Afya ya Uzazi na Mtoto na Viashiria vya Malaria wa Mwaka 2022.

Utafiti huo umeonesha sekta ya afya imeendelea kuimarika katika maeneo yote, hususan katika kupunguza vifo vinavyotokana na uzazi na kwa watoto chini ya miaka mitano.

Hayo yamesemwa jijini hapa juzi na Mtakwimu Mkuu wa Serikali kutoka Ofisi ya Taifa wa Takwimu Dkt. Albina Chuwa, wakati akitoa taarifa kuhusu utekelezaji wa shughuli za kitakwimu katika Serikali ya Awamu ya Sita katika kipindi cha miaka mitatu.

Amesema matokeo ya Utafiti huo yalionesha kuwa vifo vitokanavyo na uzazi vilipungua kwa kasi kubwa kutoka vifo 556 kwa kila vizazi hai 100,000 mwaka 2015/16 hadi vifo 104 kwa kila vizazi hai 100,000 mwaka 2021/22.

“Lengo ni kufikia mwaka 2030 wakati wa kuhitimisha Agenda 2030 ya SDGs kusiwepo na vifo vitokanavyo na uzazi,”alisema Dkt.Chuwa.

Kwa upande wa maambukizi ya UKIMWI, amesema utafiti uliofanyika matokeo yameonesha kuwa watu wenye umri wa miaka 15 na kuendelea wanaoishi na na VVU yanaendelea kupunga kutoka asilimia 4.9 Mwaka 2016/17 hadi asilimia 4.4 Mwaka 2022 hadi 2023.

“Maana yake ni kwamba Serikali ya awamu ya sita imeendelea na juhudi zake za kupambana na maambukizi ya ugonjwa UKIMWI kwa wananchi wake na hususan vijana kwa kuwawezesha zaidi kujipatia kipato chao cha mahitaji ya msingi kila siku,”amesema Dkt.Chuwa.

Aidha, katika utafiti wa kutathimni upatikanaji wa huduma za maji, alisema ambapo Takwimu rasmi za mafanikio katika Sera ya maji na kauli mbiu ya Serikali ya awamu ya sita ” Kumtua Mwanamke Ndoo Kichwani”

Amesema matokeo ya Sensa ya watu na makazi ya Mwaka 2022 yanaonesha wanawake wengi wanaongoza kaya kwa sasa kutoka asilimia 33 ya kaya zote nchini Mwaka 2012 hadi asilimia 36 mwaka 2022.

“Haya ni mafanikio makubwa kwa mwanamke kutambulika katika jamii ya Kitanzania ya kuwa mkuu wa kaya kwa kutoa maamuzi ndani ya kaya na katika vyombo vya maamuzi katika Serikali ya awamu ya sita wanawake wamepewa nafasi,”amesema.

Vilevile amesema kuwa takwimu za matokeo ya Sensa zinaonesha Kaya zinazoongozwa na wanawake wastani wa asilimia 71.4 ya kaya hizo zinatumia maji kwenye vyanzo vilivyoboreshwa kwa mujibu wa lengo la sita la SDGs.

“Haya ni matokeo chanya ya Serikali ya awamu ya sita kutayarisha Takwimu za Kiuchumi Katika kipindi cha miaka mitatu ya uongozi wa Serikali ya Awamu ya Sita, NBS imeendelea kutoa takwimu za msingi za kiuchumi na kwa kuangalia mwaka 2023 ambapo matokeo yameonesha katika kipindi cha Julai hadi Septemba 2023, Pato halisi la Taifa liliendelea kuongezeka hadi sh. trilioni 109.2 kutoka sh.trlioni 103.7 kipindi kama hicho mwaka 2022, sawa na ongezeko la asilimia 5.3.