March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Nape Nnauye: Wizara ipo mikono salama

Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online

Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Nape Nnauye amemuhakikishia aliyekuwa Waziri wa Wizara hiyo ambaye kwa sasa ni Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara Dkt. Ashatu Kijaji kuwa amekabidhi Wizara katika mikono salama na kumuahidi kuwa yeye binafsi pamoja na Naibu wake, Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu ni wanataaluma wa Habari, Mawasiliano na TEHAMA hivyo pasipo shaka anaamini wanakwenda kutimiza matarajio ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimwa Samia Suluhu Hassan na watanzania kwa ujumla.

Sambamba na Makabidhiano ya Mawaziri hao yaliyofanyika katika Ofisi za Wizara hiyo zilizopo Mji wa Serikali Mtumba pia yalifanyika makabidhiano ya Ofisi baina Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dkt. Jim Yonazi na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara hiyo ambaye ni Katibu Mkuu wa Wizara mpya ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Makundi Maalum Dkt. Zainab Chaula na kushuhudiwa na Menejimenti ya Wizara hiyo.

Nnauye amewapongeza Dkt. Kijaji na Dkt. Chaula kwa kazi nzuri walioifanya na kuwaahidi kuendeleza yale yote waliyokuwa wameanza kuyatekeleza katika harakati za kuboresha na kuendeleza Sekta ya Habari, Mawasiliano na TEHAMA nchini.

Dkt. Kijaji ameishukuru Menejimenti ya Wizara hiyo kwa ushirikiano na uwajibikaji katika kipindi cha takribani miezi minne aliyohudumu katika Wizara hiyo na kuwasisitiza kufanyia kazi masuala yote yaliyokuwa katika hatua za utekelezaji kwa kuhakikisha yanafika mwisho mzuri unaotoa majibu na utatuzi uliokusudiwa.

Kwa upande wa Dkt. Jim Yonazi Katibu Mkuu wa Wizara hiyo amesema kuwa Dkt. Kijaji na Dkt. Chaula ni wadau muhimu wa Wizara hiyo, hivyo wataendelea kushirikiana, kushauriana na kupeana fursa mbalimbali kwa lengo la kujenga na kuboresha Sekta ambazo wameteuliwa kuzisimamia

Aidha, Dkt. Chaula ameishukuru timu ya Menejimenti ya Wizara hiyo kwa ushirikiano mkubwa kwake ambapo pamoja na kuwa ni Daktari wa binadamu lakini amekuwa na weledi mkubwa wa Sekta ya Habari, Mawasiliano na TEHAMA na ataendelea kuwa mdau mkubwa wa Wizara hiyo huku akiwausia watumishi wa Wizara hiyo kuendelea kuwa wazalendo, kufanya kazi kwa bidii na kuacha alama.

Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari,Nape Nnauye akikabidhiwa nyaraka kama ishara ya kukabidhiwa rasmi ofisi ya Wizara hiyo na aliyekuwa Waziri wa Wizara hiyo Dkt. Ashatu kijaji ambaye kwa sasa ni Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara tukio hilo limefanyika Ofisini kwake Mji wa Serikali, Mtumba jijini Dodoma.
Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye akizungumza baada ya kukabidhiwa Ofisi na aliyekuwa Waziri wa Wizara hiyo Dkt. Ashatu Kijaji (kushoto), jijini Dodoma
Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, Dkt. Ashatu Kijaji akizungumza na Viongozi wa Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari wakati wa makabidhiano ya Ofisi Mtumba, jijini Dodoma.
Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye ( katikati, mstari wa mbele), Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, Dkt. Ashatu Kijaji ( wa pili kulia, mstari wa mbele) Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dkt. Jim Yonazi (wa kwanza kulia,mstari wa mbele), na Katibu Mkuu wa Wizara mpya ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Makundi Maalum Dkt. Zainab Chaula ( wa pili kushoto, mstari wa kwanza)wakiwa katika picha ya pamoja na Menejimenti ya Wizara hiyo mara baada ya makabidhiano ya Ofisi yaliyofanyika Wizarani hapo, jijini Dodoma.
Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye akiagana na aliyekuwa Waziri wa Wizara hiyo, Dkt. Ashatu kijaji ambaye kwa sasa ni Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara baada ya makabidhiano ya ofisi jijini Dodoma.