September 23, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Nape agiza umeme kupelekwa vijiji vilivyojengwa minara 

Na Ashura Jumapili,Times majira online 

Waziri wa Habari,Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Nape Nnauye,amezitaka mamlaka husika  kuhakikisha wanapeleka huduma za umeme maeneo yote ya vijiji vilivyojengwa minara pamoja na kuweka miundombinu  Bora ili kupunguza gharama za uendeshaji ambapo kwa sasa wanatumia mafuta kuendesha minara hiyo kwa gharama kubwa.

Nape, amesema hayo Julai 16,2024 baada ya kushuhudia miundombinu mibovu ya barabara katika mnara wa Chaburezi uliopo Kata ya Nyakatanga wilayani Muleba mkoani Kagera ambapo msafara wake ulipata changamoto ya kufika katika mnara huo.

Amesema lengo la Serikali ni kujenga minara 758 kwa kushirikiana na kampuni ya simu ya Vodacom na kuwafikia Watanzania waishio vijijini milioni 8.5 nchi nzima huku Mkoa wa Kagera minara 45 inaendelea kujengwa katika Wilaya mbalimbali ambapo minara 10 imekamilika na 35 inaendelea ambapo itawafikia wananchi zaidi la laki 8.

Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Mawasiliano kwa wote  Justina Mashiba, amesema  wanatarajia kujenga minara 80 mkoani Kagera kwa gharama ya zaidi milioni 80,huku zaidi ya wakazi  milioni 1.2   wakiwa wamenufaika  na  usimikwaji wa minara hiyo katika vijiji  511.

Anasema minara hiyo inajengwa na kampuni ya Vodacom kwa ufadhili wa serikali ya Jamhuri ya muungano wa Tanzania. 

Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Mawasiliano kwa wote Justina Mashiba

Akiwa Biharamulo  amesema mradi wa mnara wa Katahoka ulipo wilayani humo  uliogharimu kiasi cha  milioni 135, utahudumia vijiji vitatu ambavyo ni Katahoka,Kisuma na Nyamatongo.