September 21, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Naibu Waziri Gekul awataka Basata kuwasajili Wasanii

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online

NAIBU Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Pauline Gekul, ameitaka Bodi ya Filamu Tanzania kushirikiana na Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA), kukamilisha kwa wakati mfumo wa kielektroniki wa usajili wa Wasanii hapa nchini.

Gekul ameyasema hayo, alipokutana na kufanya mazungumzo na Menejimenti ya BAKITA na Bodi ya Filamu Tanzania ikiwa ni muendelezo wa ziara yake ya kuzitembelea Taasisi zilizo chini ya wizara hiyo.

“Hakikisheni mnawasajili na kuwafikia wasanii wote nchini ili kujua idadi yao kamili na wapi walipo ili waweze kunufaika na fursa mbalimbali ikiwamo mikopo na mafunzo ya kuwaongezea ujuzi,” amesema Gekul.

Mbali na hivyo, pia amelielekeza Baraza la Kiswahili la Taifa kuongeza kasi ya kuratibu mpango wa kuwa na vituo vya kufundishia lugha ya Kiswahili kupitia balozi zetu mbalimbali nje ya nchi.

Pia Gekul, amelitaka BAKITA kuhakikisha linafuatilia kwa karibu na kuhakikisha kuwa maelekezo ya viongozi wa Kitaifa kuhusu kubadili sheria na kanuni mbalimbali zilizo katika lugha ya kingereza kuwa katika lugha ya kiswahili yanafanyiwa kazi kwa haraka.