May 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mwambe aeleza jitihada ya serikali kuinua uwekezaji baada ya uhuru


Na Ahmed Sagaff ,Maelezo,timesmajira

Tangu Tanzania Bara ilipopata uhuru mnamo 1961, Serikali imechukua hatua mbalimbali za kuhamasisha uwekezaji nchini ili kukuza uchumi wa Taifa na kuboresha hali ya maisha ya wananchi wake.

Hayo yamesemwa jana jijini Dodoma na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Uwekezaji),Geoffrey Mwambe alipozungumza na Watanzania kupitia vyombo vya habari amesema serikali imefanya mabadiliko mbalimbali ya kisheria na kisera ambapo Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliasisi jitihada hizo kwa kusaini Sheria ya Kuhamasisha Uwekezaji wa Kutoka Nje ya nchi (Foreign Investment Protection Act) mnamo mwaka 1963.

Mwambe amezitaja sheria na sera nyingine zilizotungwa kuwa ni Sheria ya Kuhamasisha na Kulinda Uwekezaji (1990), Sera ya Taifa ya Kuhamasisha Uwekezaji (1996) na Sheria ya Uwekezaji Tanzania (1997).”kuna juhudi nyingine za kuinua sekta hiyo nchini ni uanzishwaji wa kituo cha utoaji huduma za uwekezaji, uanzishwaji wa Kamati mbalimbali za kitaifa kuhusu masuala ya uwekezaji na kuimarisha majadiliano kati ya sekta ya umma na sekta binafsi,” amesema.

Ametaja juhudi nyingine ni kufanya tafiti na tathmini za mazingira ya biashara na uwekezaji, kukuza ushiriki wa wananchi katika shughuli za kiuchumi, na kukuza ushiriki wa wananchi katika miradi ya kimkakati na uwekezaji.

Akielezea mchango wa uwekezaji kwenye uchumi,Mwambe amesema uwekezaji wa mitaji kutoka nje umekuwa ukiongezeka kutoka Dola za Marekani bilioni 0.73 mwaka 1996 hadi Dola za Marekani bilioni 2.18 mwaka 2013 na hadi Dola za Marekani bilioni 1.01 mwaka 2020.