September 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Msigwa:Muswada wa sheria ya huduma ya habari utawasilishwa Bunge lijalo kutokana na ufinyu wa muda

Na Zena Mohamed,TimesMajiraOnline,Dodoma.

MSEMAJI Mkuu wa Serikali ,Gerson Msigwa amesema kuwa Serikali ilikusudia kupeleka muswada wa Sheria ya Huduma ya Habari namba 12 ya mwaka 2016 kwenye mkutano wa 10 katika bunge ambalo linaendelea ili uweze kujadiliwa lakini kutokana na muda kuwa mdogo hautaweza kuwasilishwa mpaka bunge lijalo ambalo linatarajiwa kuwa mwezi wa nne.

Msigwa amesema hayo jijini hapa leo,Februari 7,2023 wakati akizungumza na waandishi wa habari ambapo amesema kutokana na ufinuyu wa muda wa shughuli za bunge zinazoendelea hapa mjini Dodoma kwa wabunge kujadili taarifa ya kamati za kudumu za bunge imepelekea kusogeza mbele mswada wa Sheria ya huduma ya Habari uliofanyiwa marekebisho kutopelekwa bungeni kujadiliwa kama ilivyo stahili kuwa.

“Kama mnavyojua ndugu zangu wana habari Serikali baada ya kusikiliza maoni mbalimbali kutoka kwa wadau wa habari walitaka sheria ya huduma ya habari kufanyiwa marekebisho na kweli serikali ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassani aliona ni jambo jema ili kila mmoja aweze kufurahi na huduma hiyo,

“Kweli serikali imekusanya maoni na hata wanahabari walitoa maoni yao kwa kutokana na kupatikana mwa maoni Serikali ilikuwa imekusudia kupereka marekebisho hayo bungeni ili wabunge waweze kujadili mswada huo,

“Lakini kama mnavyojua kwa sasa bunge hili linaloendelea ni kwa ajili ya kujadili taarifa za kamati za bunge na kwa maana hiyo muda haukuweza kutosha kuweza kujadili mswada huu kwa maana hiyo basi mswada huo mahususi kama “Jambo letu”hautaweza kupelekwa bungeni lakini tunauhakika kwamba bunge lijalo la mwezi wa nne mswada huo utapelekwa bungeni na utajadiliwa kwani huko vizuri na umeandaliwa vizuri,”amesema Msigwa.

Hata hivyo Msigwa amesema Maoni yote ya wadau yamezingatiwa na yamefanyiwa kazi kwani wanataka mswada huo uweze kuwafurahisha watanzania wote ili kila mdau wa habari aweze kuwa na uhuru wa sheria hiyo na hiyo ndiyo makusudi njema ya serikali.

Pamoja na hayo amesema kuwa ukiacha Sheria ya Huduma ya Habari bado kuna miswada mingi ambayo ilitakiwa kupelekwa bungeni lakini kutokana na ufinyu wa muda miswada hiyo haikuweza kupelekwa bungeni na yote itapelekwa bungeni katika bunge lijalo kwa manufaa ya watanzania wote.