May 16, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Miaka mitatu ya Rais Samia yachochea huduma za afya hospitali ya rufaa ya mkoa

Na Esther Macha, Timesmajira Online, Mbeya

HOSPITALI ya Rufaa ya Mkoa wa Mbeya imeongeza idadi ya kupokea wagonjwa kutoka 57,000 mpaka 132,000 kwa kipindi cha miaka mitatu hali inayoelezwa kuwa ni kutokana na maboresho yaliyofanywa na Rais Dkt .Samia Suluhu Hassan katika sekta ya afya.

Miaka ya nyuma walikuwa wakipokea wagonjwa 4,800 kwa mwezi na baada ya Serikali kuboresha miundombinu idadi ya wagonjwa imeongezeka na kufikia 11,000.

Mganga mfawidhi hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mbeya Dkt.Abdallah Mmbaga akitoa taarifa kwa waandishi wa habari

Akizungumza Machi 22,2024 na Waandishi wa Habari wakati akitoa taarifa ya miaka mitatu ya uongozi wa Rais Samia Mganga Mfawidhi wa HospitalI ya Rufaa ya Mkoa wa Mbeya,Dkt.Abdallah Mmbaga amesema kuwa katika uboreshaji wa hospitali hiyo umeleta matokeo chanya ambapo wameimarisha ustawi wa jamii katika hospitali hiyo hususani kwa wananchi wa mkoa huo.

“Uboreshaji huo lengo kuu ni kuhakikisha kuwa kila mwananchi anapata huduma bora za afya ambazo watazipata kwa ukaribu,”amesema Dkt.Mmbaga.

Pia ameeleza kuwa hospitali imeajiri wafanyakazi wapya takribani 34 kwa kipindi cha miaka mitatu cha uongozi wa Rais Samia namkufanya kuwa na watumishi 410 wakiwemo wa mkataba takribani 83.

Aidha ameeleza kuwa kumekuwa na upatikanaji wa dawa na vifaa tiba vya kutosha na imeongeza uwezo wa hospitali kutoa huduma bora za matibabu kwa wagonjwa na ongozeko la bidhaa katika kipindi cha miaka mitatu kutoka asilimia 78 mwaka 2022 hadi asilimia 89 kufikia mwaka 2024.

“Kwa kipindi hicho hospitali ilipatiwa zaidi ya bilioni 4 kwa ajili ya ujenzi wa ICU na vifaa vyake,nyumba ya mtumishi,ununuzi wa Digital X_Ray na CT_Scan huku kiasi cha bilioni 7 zimetumika kwa ajili ya kukamilisha mradi wa jengo la kisasa la upasuaji,”ameeleza.

Jengo la upasuaji katika hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mbeya

“Naona ni vitu vingi vimeboresha katika kipindi hichi cha miaka mitatu ya Rais Samia kuanzia kwa mama na mtoto kuliko huko nyuma kwa sababu hata mgonjwa akifika hospitali huduma zilikuwa tofauti na vipimo vingi vilikuwa hamna ambapo ilitulazimu kwenda nje ya Mkoa kufuata huduma hiyo,”amesemaMkazi wa Nzivwe jijini Mbeya Mulungu .