March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mhandisi wa Maji akutwa amejinyonga kwa manila

Na Eliasa Ally, Iringa

MHANDISI wa Maji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi mkoani Songwe, Stephan Sengayavene (55) amefariki baada ya kujinyonga katika chumba ambacho alikuwa amelala kwa kutumia kamba ya manila.

Sengayavene alikuwa amelala katika chumba cha nyumba ya mdogo wake alipokuwa amekwenda kumtembelea, Mwalimu Oscar Sengayavene anayeishi katika Kijiji cha Kinegembasi katika Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi Mkoa wa Iringa.

Akizungumza ofisini kwake na Majira, Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Iringa, RPC Juma Bwire amesema kuwa, marehemu Stephan Sengayavene alijinyonga April 27, 2020 majira ya saa 07:15 asubuhi katika Kitongoji cha Shuleni “A” Kijiji cha Kinegembasi kilichopo Kata ya Itandula Tarafa ya Kisanga wilayani Mufindi Mkoa wa Iringa.

Kamanda Bwire amesema kuwa, Stephan Sengayavene ambaye kabila lake ni Mhehe anafanya kazi ya uhandisi katika wilaya ya Mbozi katika mkoa wa Songwe ambapo alifanya safari kuja kumtembelea mdogo wake ambaye ni mwalimu katika wilaya ya Mufindi katika kijiji cha Kinegembasi.

“Marehemu Sengayavene alikutwa amefariki dunia kwa kujinyonga kwa kutumia kamba ya manila ya rangi ya kijani na mwili wake ulikutwa ukiwa umening’inia kwenye dari chumbani alikokuwa amelala katika chumba cha nyumba ya mdogo wake anayeitwa Oscar Sengayavene ambapo alikuwa amefikia,”alisema Kamanda Bwire.