March 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mgogoro wa shamba miaka 17 wafikia tamati

·Ni kwa mkorea Kigamboni, wananchi kicheko

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira,Online,Dar

MGOGORO wa shamba lenye ukubwa wa ekari 302 maarufu kama kwa mkorea Kigamboni jijini Dar es Salaam ambao umedumu kwa miaka 17 hatimaye umefikia tamati.

Hatua hiyo ilitangazwa jana na Meya wa Manispaa ya Wilaya ya Kigamboni, Ernest Mafimbo, wakati akizungumza na waandishi wa habari baada ya kikao cha Maalum Baraza la Madiwani.

Meya alisema mgogoro wa eneo hilo lenye ukubwa wa ekari 302 ulianza mwaka 2004 na umedumu kwa muda mrefu sana kutokana na mvutano uliokuwepo baina ya wananchi na mwekezaji.

Meya alisema jana kuwa baada ya vuta vikuvute ya miaka yote hiyo sasa imekubaliwa mwekezaji huyo abaki na ekari 150 na wananchi wapewe ekari 152.

Alisema mgogoro huo wa muda mrefu umepitia hatua mbalimbali za utatuzi kuanzia wilaya, Mkoa Mahakama Kuu lakini hakukuwa na ufumbuzi wowote.

“Ilipofika wizarani yenyewe ilileta maelekezo kuitaka Manispaa ya Kigamboni kwamba baada ya kutoa tamko lake kuwa kiwanja cha wakorea mission ekari 302 eneo ambalo kwa asili lilikuwa linagombaniwa na wananchi na mwekezaji,” alisema

“Wizara ikaamuru wananchi wabaki na ekari 152 na mwekezaji huyo abaki na ekari 150 Manispaa ilipewa jukumu la kusimamia kuhakikisha hili linafanikiwa bila kuwa na tatizo lolote,” alisema

Alisema wananchi hao walishauri atafutwe mtu binafsi ambaye wanamwamini kwaajili ya kupima viwanja hivyo na manispaa iwe kati ili mwisho wa siku mtaalamu huyo apime viwanja vyao.

“Mawazo yao tuliyapitisha kwasababu lengo letu kubwa ilikuwa kuwaondolea kero wananchi hatukuwa na maslahi binafsi hivyo tulikubali matakwa yao kwasababu wao waliona tukifanya hivyo watapata haki,” alisema

Alisema baraza limebariki viwanja hivyo viuzwe kwa kupitia mtaalamu huyo ambaye wananchi hao wamemwamini na kumpendekeza na Manspaa itasimamia kuhakikisha kila mwananchi anapata haki yake na hakuna mtu anadhulumiwa.

Alisema mtaalamu huyo anaitwa Gombo Samandito ambaye amefanya mchakato wa kuchonga barabara, michoro iliyotoka kwenye viwanja hivyo kuweka mawe na kuhakikisha eneo zima limepimwa.

“Kwa hatua hii sisi Baraza la Madiwani tutafuatilia kuhakikisha kila kitu kinakwenda sawa kuhakikisha wananchci wote wanapata haki zao na hakutakuwa na malalamiko tena,” alisema

Mmoja wananchi wanaotarajiwa kunufaika na viwanja hivyo, Mwajuma Omari aliishukuru serikali kwa kuhakikisha mgogoro huo wa muda mrefu unafikia tamati.

“Napenda sana kuwashukuru madiwani na meya kwa kuamua kumaliza tatizo hili, tumevumilia sana tangu mwaka 2004 nenda rudi lakini leo hii tumeambiwa kwamba mgogoro umeisha tunashukuru sana,” alisema

Maua Omari ambaye naye ni mnufaika wa eneo hilo alisema mwekezaji huyo mwaka 2006 waliwapa fedha ndogo kiujanja ujanja kwa lengo la kutwaa eneo hilo lakini baadaye wananchi waligoma kuondoka.

“Mwekezaji alipokuja mwaka ule hakuwa na utaratibu mzuri wa kuwalipa wananchi yeye alikuwa anakuangalia akiona mzee sana anaweza kukupa hata Sh 50,000, sasa mimi nilikuwa na ekari 1.5 lakini alinipa Sh 100,000 ndiyo sababu wananchi wakaamka na kuanza kudai haki yao,” alisema

Mwish