May 2, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Meya Kumbilamoto asaini mikataba ya barabara ya zege, Lami

Na Heri Shaaban, TimesMajira Online, Ilala

MEYA wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam Omary Kumbilamoto ,Leo amesaini mikataba kwa Kampuni za Wakandarasi watakajenga Barabara za viwango vya zege na Lami Wilayani Ilala .

Mikataba hiyo Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam Omary Kumbilamoto, amesaini katika ukumbi wa Mikutano Arnatogluo halmashauri ya Jiji ambapo wameshuhudia viongozi wa chama Cha Mapinduzi Mwenyekiti Said Sidde, na Mkuu wa Wilaya Edward Mpogolo na Watendaji wa Halmashauri .

“Naipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan, tunaomba Mkuu wa Wilaya Edward Mpogolo utufikishie salam zetu kwa Rais kuwapatia Mradi wa awamu ya pili wa kuboresha Miundombinu ya Jiji (DMDP) mradi wa DMDP ukianza na kumalizika utakuwa mkombozi mkubwa wa Barabara za ndani katika Halmashauri ya Jiji “alisema Kumbilamoto .

Meya Kumbilamoto alisema Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini TARURA ni wasanifu na wasimamizi Wakuu wa Barabara zote za Wilaya ya Ilala .

Alitaja Barabara zitakazo jengwa kwa kiwango cha zege Barabara Mtendeni na Southern Jimbo la Ilala K.M 02 ,Barabara za kiwango cha Lami Nyati,Rufiji ,Mchikichi KM 1.04 ambazo zitagharimu shilingi Bilioni 1,916 ,245,530 .

Aidha alisema katika Jimbo la Ukonga Barabara zitakazo jengwa kiwango cha Lami Pugu Majohe KM 0.4 Kitunda Kivule KM 0.5 na Mpalange Mwanagati KM 0.5 gharama ya ujenzi shilingi Bilioni 1.97 .

Meya Kumbilamoto aliwataka wakandarasi waliopata tenda ya ujenzi wa Barabara hizo za ndani Halmashauri ya Ilala KUJENGA kwa muda wa miezi sita wawe wamemaliza ujenzi wa Barabara hizo .

Alitoa agizo kwa wakandarasi waliopewa tenda ya ujenzi marufuku kuuza vifusi vyote vinaitajika katika kuziba Barabara korofi.

Alisema usanifu wa Barabara hizo zinazojengwa wamewashirikisha wabunge na madiwani wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam .

Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji Amani Mafuru, alisema Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan, alitoa Maelekezo kwa halmashauri zote nchini imekuwa ikitenga asilimia kumi ya ujenzi wa Barabara za ndani ,fedha hizi zinajenga barabara za majimbo yote matatu na Wakandarasi wamefuata taratibu leo wamesaini mikataba .

Mkuu wa wilaya ya Ilala Edward Mpogolo alisema shilingi bilioni 6.2 za Barabara wilayani Ilala aliwapongeza Meya wa Halmashauri ya Jiji Omary Kumbilamoto ,Wabunge na madiwani wa Halmashauri kwa usimamizi mzuri na kuitikia maagizo ya Rais Dkt .Samia Suluhu Hassan.

Mkuu wa Wilaya Edward Mpogolo alitoa agizo kwa Wakala wa Barabara Mijini na Vijijini TARURA kuakikisha wanaenda kusimamia barabara zote ambazo zinajengwa .

Mwenyekiti wa chama Cha Mapinduzi CCM Wilaya ya Ilala Said Sidde alipongeza Halmashauri ya Jiji kwa kusaini mikataba ya ujenzi wa Barabara za kisasa kwa uwazi na ukweli ambapo alitoa wito kwa wakandarasi watimize yale yalio katika mikataba .