May 5, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Katibu Mkuu wa CHADEMA, John Mnyika, akizungumza na waandishi wa habari Makao Makuu wa CHADEMA Kinondoni Jijini Dar es Salaam

Mchakato wa waomba Urais CHADEMA waelekea ukingoni

Na David John, TimesMajira Online, Dar es Salaam

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kimesema mchakato wa kupitia fomu za makada wa chama hicho waliojitokeza kugombea urais upo katika hatua za mwisho kukamilisha.

Chama hicho kimesema mara baada ya mchakato kukamilika, utaratibu wa kuchukuwa fomu hizo za urais ikiwamo na za ubunge,udiwani utatangazwa na kuwekwa hadharani.

Katibu Mkuu wa CHADEMA, John Mnyika, akizungumza na waandishi wa habari Makao Makuu wa CHADEMA Kinondoni Jijini Dar es Salaam

Akizungumza na waandishi wa habari Makao Makuu wa CHADEMA Kinondoni Jijini Dar es Salaam jana, Katibu Mkuu wa CHADEMA, John Mnyika, pamoja na mambo mengine amesema mchakato wa kupitia fomu za wagombea urais upo katika hatua za mwisho, lakini chama kitapanga siku nyingine za kuzungumzia suala hilo.

Hata hivyo, alielezea kusikitishwa kwake na kauli ya Mkuu wa Jeshi la Polisi ncjini, IGP Simon Sirro, ya kuwaonya wanasiasa wanaosema watalinda kura zao. Mnyika amesema wao kama chama watalinda Kura zao kwa nguvu ya umma.

Wakati huo huo CHADEMA imelitaka Jeshi la Polisi nchini kuonesha ushahidi wa CCTV Kamera ili kuthibitisha madai kuwa Mwenyekiti wa Chama hicho, Freeman Mbowe alilewa kama ambavyo ilielezwa na Jeshi hilo.

“Mwenyekiti Freeman Mbowe alishambuliwa na alipata madhara katika moja ya sehemu za mwili wake, lakini mbaya zaidi Jeshi la Polisi limeendelea kukaa kimya na badala yake wanatoa taarifa  ambazo hawana ushahidi.

Tunalitaka Jeshi la Polisi kujitokeza hadharani na kutoa ushahidi wa CCTV Kamera, “amesisitiza Mnyika “Kwa nini Jeshi la Polisi wanashindwa kuja na majibu wakati madaktari ambao walimpokea Mwenyekiti Mbowe wangeweza kutoa ushahidi.”

Amesema suala hilo linahitaji ushahidi vinginevyo ni kuendelea  kuwachafua viongozi wa chama hicho kwa wananchi katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu.