May 4, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mbunge aomba walimu waruhusiwe kuwafuata wenza wao

Na Joyce Kasiki,Dodoma

MBUNGE wa Viti Maalum Sophia Mwakagenda (CHADEMA) ameiomba Serikali iwaruhusu walimu wanawake na wanaume wawafuate wenza wao kwa lengo la kutunza maadili lakini pia kulinda ndoa zao.

Akiuliza swali la nyongeza Feb 8 mwaka huu  Bungeni jijini Dodoma ,Mwakagenda amesema suala la walimu  kufuata wenza wao ni la muhimu sana kifamilia.

“Je  serikali inaonaje kuhakikisha wale ambao wamefunga ndoa wawafuate wenza wao ili kuepuka na changamoto mbalimbali zikiwemo za maambukizi ya magonjwa”?amehoji Mwakagenda

Akijibu swali hilo Naibu Waziri Ofisi ya Rais,Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Deo Ndejembi amesema ,walimu hao wanaruhhsiwa kuwafuata wenza wao lakini kwa kufuata sheria,taratibu na miongozo ya Utunishi wa umma iliyowekwa.

“Utumishi wa umma unaongozwa kwa sheria kanuni , taratibu na miongozo mbalimbali ya utumishi wa umma,na mtu anapokuwa ameajiriwa katika utumishi wa umma anafuata hayo yote ,

“Sheria inasema atafanya kazi mwaka mmoja kisha atafanyiwa ‘assessment’ na kuthibitishwa kazini ,baada ya kuthibitishwa kazini ni lazima atumikie nafasi kwa muda usiopungua miaka miwili katika lile eneo ,

“Baada ya hapo anaruhusiwa kuomba uhamisho kwenda eneo lolote nchini ingawa inategemea na nafasi ya kule anakotaka kwenda kama ule mshahara wake je bajeti imetengwa kwa yule mwajiri anakotaka kuhamia.”