May 17, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Makonda kukutana na TAKUKURU ana kwa ana kumaliza rushwa Muleba

Na Jackline Martin, TimesMajira Online, Muleba

KATIBU wa NEC, Itikadi na uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM),Paul Makonda amesema atazungumza na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), kuweka timu maalumu kuhakikisha suala la Rushwa lililokithiri Wilaya ya Muleba linaisha .

Makonda ameyasema hayo leo,Novemba 10,2023,wakati akizungumza na wananchi wa Wilaya ya Mulemba Mkoa wa Kagera ikiwa ni muendelezo wa ziara yake mikoa ya Kanda ya ziwa akianzia Kagera.

“Muleba kuna harufu ya rushwa kwenye vitalu, ofisi za utumishi wa umma, kituo cha polisi, nitaongea na Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU na kuweka timu maalumu kuhakikisha kwamba rushwa siyo sehemu ya Wilaya ya Mulemba,” amesema

Akizungumzia Changamoto ya maji Wilayani hapo, Makonda amesema atazungumza na Waziri wa Maji, Juma Aweso, kuhakikisha Mulemba wanapata maji na kuondoa kero wanayoipata wananchi.

“Kabla ya sijamaliza mkutano wangu Chato, nitakuwa nimeshaongea na Waziri wa maji na ataniambia mpango uliopo kuhakikisha Muleba mnapata maji,

“Mambo ambayo Rais Dkt.Samia ameyafanya na fedha anazozileta hapa tunataka zisimamiwe vizuri ili kukamilisha utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi,

Makonda ameongeza kuwa “Kazi ikifanyika kwa uaminifu na watumishi wakipokea fedha ikaenda kwenye mradi uliokusudiwa, kama ni mradi wa Barabara tunataka kuona ubora wa kiwango cha lami Cha ujenzi wa Barabara,”alisema.

Katika hatua nyingine makonda amewataka viongozi wa CCM,Wilaya ya Mulemba Mkoa wa Kagera kukamilisha ujenzi wa ofisi ya Chama lakini pia kuhakikisha mapato ya Chama yanajulikana.

Makonda amesema wakati wa Chama kusikiliza wanyonge, kuwa mtetezi wa mkulima na mfugaji na kupigania maslahi ya wanyonge umefika.