March 7, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Makonda ateuliwa Waziri wa Habari, Simbachawene atenguliwa Uwaziri  

Na Mwandishi Wetu, Timesmajira Online

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dkt. Samia Suluhu Hassan,amemteua Paul Christian Makonda (Mb.) kuwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo. 

Ambapo kabla ya uteuzi huu,Makonda alikuwa Naibu Waziri katika Wizara hiyo,hivyo amechukua nafasi ya Prof. Palamagamba Kabudi (Mb.) aliyekuwa Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo ambaye kwa sasa ameteuliwa kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Ikulu (Kazi Maalum). 

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Dkt. Moses Kusiluka, Rais Samia amefanya uteuzi na utenguzi  wa viongozi Januari 8,2026.

Pia Rais Samia amemteua Patrobas Katambi kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi ambaye alikuwa Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara kabla ya uteuzi huo akichukua  nafasi ya Boniface  Simbachawene  ambaye uteuzi wake umetenguliwa.

Huku Dennis  Londo,ameteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara ambaye kabla ya uteuzi huo alikuwa Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi.

Aidha Ayoub Mahmoud  ameteuliwa kuwa Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi huku Dkt. Richard Muyungi ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira). Dkt. Muyungi anachukua nafasi ya Mhandisi Cyprian  Luhemeja ambaye ameteuliwa kuwa Balozi.

Mbali na hao pia Rais Samia amemteua Mhandisi Zena  Said  kuwa  Balozi,

Waziri Rajab Salum ameteuliwa kuwa Balozi na  Meja Jenerali Mbaraka Mkeremy ameteuliwa kuwa Balozi.

Hata hivyo Mhandisi Samaje ameteuliwa kuwa Ofisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) akichukua nafasi ya Dkt. Mussa Budeba.

Vile vile uteuzi wa Prof. Eliakimu Mnkondo Zahabu, Mwenyekiti wa Bodi ya Kituo cha Taifa cha Ufuatiliaji wa Kaboni (NCMC) umetenguliwa.

Haya hivyo  uapisho wa viongozi wateule utafanyika Januari 13, 2026 Ikulu Chamwino, Dodoma kuanzia saa 8.00 mchana.