April 30, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Madiwani wa Viti Maalum Ilala watoa msaada hospitali ya Ocen Road

Na Heri Shaaban, TimesMajira Online

MADIWANI wa viti Maalum Wanawake Halmashauri ya jiji la Dar es Salaam wametoa misaada ya vitu mbali mbali kwa ajili ya kusaidia wagonjwa waliolazwa katika hospitali wagonjwa wa Salatani Ocean Road iliyopo wilayani Ilala.

Misaada hiyo ya vifaa hivyo vilitolewa leo Madiwani wa wilaya ya Ilala walifanya ziara hospitali hapo kuona wagonjwa waliolazwa katika hospitali hiyo.

Akikabidhi misaada hiyo kwa niaba ya madiwani wa viti Maalum Wilaya ya Ilala Katibu wa Madiwani wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, Diwani Moza Mwano alisema,madiwani wanawake wameguswa kwa umoja wao wameungana pamoja kwenda kuona wagonjwa kuwafariji na kutoa misaada hiyo.

Diwani Moza alisema kuna watu wengi wamelazwa katika hospitali hiyo hawana ndugu hivyo misaada hiyo itawasaidia katika kutolea huduma mbalimbali .

“Sisi Madiwani wa Halmashauri ya jiji la Dar es Salaam tumeweka utaratibu wetu kutembelea makundi maalum, kutembelea watoto wa mahitaji Maalum kila mwaka mwaka huu tumetembelea kutoa misaada katika hospitali ya Ocean Road katika hospitali hii kuna watu mbali mbali wamelazwa na wengine hawana ndugu.

Diwani Moza Mwano alitumia fursa hiyo kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan kwa kuwekeza katika sekta ya afya kwa kujenga vituo vya afya vya kisasa na hospitali kwa ajili ya kusaidia wananchi waweze kupata huduma bora karibu na makazi yao.

Alisema pia katika hospitali hiyo kuna wanawake wezao ambao wamepatwa na shingo ya uzazi ambapo aliwataka wadau mbalimbali kujitokeza kusaidia sekta ya afya katika kuunga mkono juhudi za Serikali.

Diwani Viti Maalum Wilaya ya Ilala, Semeni Mtoka alianza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu na kutoa wito kwa watanzania na taasisi mbalimbali kutoa misaada ikiwemo ya nguo .

Diwani Semeni Mtoka alisema madiwani wa Ilala wanaendelea kushikana pamoja katika kusaidia utekelezaji wa Ilani unaofanywa na Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan kwenye sekta ya afya.