May 4, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Lukiza Autism yazindua Jezi mpya ya Run4Autism 2024

Na Penina Malundo, timesmajira

TAASISI ya Lukiza Autism inayoandaa mbio za kuelimisha jamii kuhusu usonji ”Run4Autism Tanzania”imezindua rasmi jezi za mbio hizo kwa mwaka 2024 watanzania watakaojitokeza katika kukimbia katika mbio hizo Aprili 28 mwaka huu.

Akizungumza hayo jana wakati wa uzinduzi wa Jezi hizo,Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi hiyo,Hilda Nkabe amesema katika jezi hizo zipo aina tatu rangi ya njano  iliyochanganywa na kijani,nyekundu iliyochanganywa na nyeupe pamoja na rangi ya bluu iliyochanganywa na nyeupe.

Amesema mwaka huu ni msimu wa tatu wa mbio hizo ambazo zinatarajia kufanyika Aprili 28 mwaka huu katika viwanja vya farasi lengo ikiwa ni kutoa elimu kwa jamii kuhusu usonji,kuleta wadau katika eneo moja wakiwemo wazazi,vituo vya kulelea watoto,vituo vya kutolewa mazoezi tiba pamoja na serikali na wadau.

Nkabe amesema  katika mbio hiyo itakuwa na route nne ambapo Kilomita 21.1,Kilomita 10 ,Kilometa 5 na 2.5 ambapo inawahusisha watoto wadogo na watu wenye ulemavu kwani mbio hizo ni jumuishi na ya kifamilia.

Amesema gharama za usajili wa mbio hizo ni 35000 kwa mtu mmoja ambapo atapata vifaa vyote vya kukimbia ikiwemo  Tshirt,Medali, pamoja na Begi ambapo bei hii inakuwa ya punguzo hadi Aprli 2,2024 na kuanzia Aprili 3,2024 bei itakuwa 45000.

”Kuanzia hapo gharama itaongezeka na kuwa 45000 hii inatokana na kugharamia gharama za vifaa vya kushiriki na kutenga fedha kidogo kuingiza katika mradi wetu wa mwaka huu wa kuwaongezea uwezo walimu wa chekechekea kuweza kutambua viashiria  za mtoto mwenye usonji tangu anapokuwa mdogo,”amesema.

Kwa Upande wake Meneja wa Kituo cha Spark Rehabilitation kinachosaidia watoto wenye usonji katika kuwapa mazoezi, Epifania Mrosso amesema mbio hizo zitasaidia kwa kiasi kikubwa wazazi wa watoto wenye usonji kuendelea kuwatoa nje watoto wao na sio kuwaficha.

Amesema watoto hao wanaweza kutengenezewa uwezo wa kujitegemea na kujiamini.”Tunaungana na Lukiza Foundation katika mbio hizi katika kuwasaidia watoto wenye usonji kutolewa nje na sio kufungiwa ndani hivyo lazima jamii inapaswa kupewa elimu ya kutosha,”amesema.