May 22, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Liquid yatambulisha toleo la pili Azure Stack

Na Agnes Alcardo, Timesmajira Online, Dar es Salaam

Kampuni ya Liquid Intelligent Technologies ambayo ni sehemu ya Cassava Technologies pamoja na makampuni ya kiteknolojia ya Kiafrika kwa kushirikina na wingu africa, imetambulisha toleo la pili la huduma ya Azure Hyperconverged Infrastructure (HCI).

Uwekezaji huo kutoka Liquid Tanzania, utatoa mazingira bora zaidi kwa wafanyabiashara wa ndani kuongeza kasi ya safari yao ya kubadilika kidigitali.

Akizungumzia hilo Jijini Dar Es Salaam mwisho mwa wiki,Kaimu Afisa Mtendaji Mkuu wa Liquid Intelligent Technologies Tanzania, Manish Govindji alisema mwaka 2021 Liquid walikuwa wa kwanza kuleta huduma ya Azure Stack kwa wafanyabiashara hapa nchini.

“Mwaka 2021, tulikuwa wa kwanza kuileta huduma ya Azure Stack kwa wafanyabiashara wa Kitanzania, kuwasaidia kupata suluhisho la kuhifadhi taarifa kwa njia ya mtandaoni ili kukidhi mahitaji ya sheria za ndani za kudhibiti data na kuendesha kwa ufanisi wa programu za biashara zinazohitaji mtandao wenye kasi.

“Hii ni hatua nyingine muhimu tuliyofanikiwa kuifikia wakati tunaendelea na jitihada za kuwawezesha wateja wetu kuanza kutumia teknolojia ya kuhifadhi taarifa zao mtandaoni na kuchangia kuifanya Tanzania kuwa na uchumi wa kidigitali,” amesema Manish Govindji.

Hata hivyo amesema, Suluhisho pekee linalotolewa na Azure Stack HCI, linahakikisha kuwa biashara zinakidhi viwango vya ubora vya ndani kwa kuruhusu wateja kuendesha programu zilizoundwa kwa miundombinu iliyoboreshwa kidigitali.

Pia amesema kuwa, kwa kutoa huduma isiyo na upendeleo wa mtandao kutoka ‘Wingu Group’, makampuni yanayo fursa zaidi ya kuchagua mtoa huduma wa mtandao wa mawasiliano.

Ameongeza kuwa, kundi la makampuni ya Wingu linayofuraha kushirikiana na Liquid Intelligent Technologies kutambulisha awamu ya pili ya huduma ya Azure Stack nchini Tanzania, hatua muhimu katika kuongeza kasi ya mageuzi ya kidigitali kitaifa.

“Kwa kuwapatia wafanyabiashara wa ndani upatikanaji wa suluhisho la huduma za ubora wa viwango vya juu la kuhifadhi taarifa mtandaoni, tunalenga kuwawezesha kufanikiwa katika zama hizi za kidigitali.

“Kituo chetu cha data isiyo na upendeleo wa mtandao kinachangia kufanikisha juhudi hizi, kuyawezesha makampuni kuchagua mtoa huduma wanayempendelea.

“Kwa kushirikiana pamoja na Liquid, tunachangia katika uchumi wa kidigitali wa Tanzania, kukuza uhusiano wa kiuchumi, na kutengeneza usawa kwenye sekta ya teknolojia kwa biashara za ndani.

“Ushirikiano huu unaonyesha mafanikio ya hatua muhimu katika kupanua upatikanaji na unafuu wa teknolojia nchini Tanzania.

“Tunatarajia kuona ongezeko la uunganishwaji, ubunifu, na ukuaji siku zijazo katika ukanda huu,” amesema Nicholas Lodge, Mwanzilishi Mwenza na Mkuu wa Mikakati wa wingu.africa.

Nicholas alisema, Uwekezaji endelevu wa Liquid katika kusambaza mtandao wake wa faiba na kuboresha upatikanaji wa suluhisho la huduma nafuu za kidigitali ni muhimu katika kuboresha mageuzi ya kidigitali nchini Tanzania na barani kote kwa ujumla.

Pia, alisema, kuhakikisha wafanyabiashara wa ndani wanaunganishwa na mtandao wenye kasi na huduma za kidigitali zinazochangia uhusiano wa kiuchumi na kiteknolojia katika nchi zote.

“Kwa kuwepo kwa toleo la pili la Azure Stack katika ukanda huu, kwa mara nyingine tena Liquid inawahakikishia kuwa ni sehemu moja ya uhakika na kuaminika kwa mahitaji yote ya teknolojia. Hasa ikizingatiwa kuwa mojawapo ya vikwazo vikubwa vya matumizi ya huduma za kuhifadhi taarifa mtandaoni nchini Tanzania ni gharama kubwa ya upatikanaji wa suluhisho zake.

“Liquid, imesambaza huduma ya Azure Stacks katika nchi tofauti Afrika, na tunao wataalamu ndani ya kampuni wanaohitajika na wateja wetu kuhakikisha kuwa mahitaji yao yote ya huduma za TEHAMA yanapatiwa ufumbuzi wakati wao wakiendelea kujikita katika shughuli zao za biashara za kila siku,” amesema Govindji.