May 17, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Naibu Spika wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,Dkt.Tulia Ackson

LHRC nayo yapongeza uamuzi wa Serikali awamu ya sita miswaada kupelekwa Bungeni

KITUO cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kimeipongeza Serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, kwa kusikiliza kilio cha miaka 30 cha wadau wa demokasia na hatimaye kuridhia kupeleka miswada mitatu Bungeni.

Miswada hiyo ni pamoja na mswaada Sheria ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi, Mswada wa Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani pamoja na Mswada wa Mabadiliko ya Sheria ya Vyama vya Siasa na Sheria ya gharama za uchaguzi yote ikiwa ya mwaka 2023.

Akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Dkt Anna Henga, amesema miswada hiyo ni muhimu katika demokrasia nchini.

Amesema kwa miaka zaidi ya 30 sasa tangu kuanzishwa kwa mfumo wa vyama vingi, Serikali imeridhia madai ya muda mrefu kutoka kwa wadau wa demokrasia ya vyama vingi chini kwa kuwasilisha miswada hiyo Bungeni.

“Katika miswada hii kuna baadhi ya mambo ambayo ni ya kupogezwa mfano suala la mgombea kutopita bila kupingwa, kuanzishwa kwa kamati ya usaili kwa wajumbe wa Tume ya uchaguzi na maamuzi ya Ofisa mwandikishaji kupingwa mahakamani,”alisema Dkt. Henga

Amesema kwa upande Mswada wa Sheria ya Vyama vya Siasa ni moja ya jambo la kupongezwa, kwani uwepo wa kifungu cha ujumuishaji wa wanawake na watu wenyewe ulemavu katika nafasi za uongozi ndani ya vyama vya siasa.

Dkt Henga ameeleza kuwa mswaada huo umependekeza kuongezwa kwa kifungu kipya cha 10C(1)(b)(c) kinachowekeza takwa la lazima kwa vyama vya siasa kuwa na sera ya ujumuishaji wa wanawake na watu wenye ulemavu katika nafasi za uongozi ndani ya vyama vya siasa.

Hata hivyo, Dkt Henga alisema mbali na mafanikio katika miswada hiyo, bado yapo mapungufu ambayo LHRC imeweza kuyabaini kuwa ni pamoja na mswada wa Sheria ya Tume ya Taifa ya uchaguzi wa mwaka 2023, Mkurugenzi wa Uchaguzi kuwa Katibu wa Kamati ya Usaili, mswada wa sheria ya Tume ya Taifa ya uchaguzi wa mwaka 2023 pamoja na Mkurugenzi wa uchaguzi kuwa Katibu wa Kamati ya Usaili.

Ameendelea kueleza kuwa eneo jingine ni watumishi wa umma kuendelea kuwa sehemu ya Tume, Tume kuendelea kutegemea bajeti ya Serikali,Tume kushauriana na Waziri mwenye dhamana na masuala ya utumishi kuandaa muundo wa utumishi wa Sekretariati ya Tume .

Hata hivyo Dkt Henga mapungufu mengine ni kigezo cha mtu kuwa Ofisa mwandamizi katika utumishi wa umma ili kuteuliwa kuwa Mkurugenzi wa uchaguzi, mpiga kura aliyepoteza au ambaye kitambulisho chake Cha kupigia kura kimefutika au kimeharibika hatapata kitambulisho kingine isipokuwa kama atalipia ada itakayoanisha na Tume.

“Mbali na mapungufu haya LHRC tunatoa mapendekezo ya jumla kwenye Mswada wa Sheria ya Uchaguzi wa Rais, wabunge na madiwani, ujumuishe haki ya wafungwa kupiga kura kwa utaratibu utakaoweka sheria,”amesema.

Amesema muswada huo, uwekewe kifungu kinachotoa haki kwa Watanzania waishio nje ya nchi (Diaspora) kuwa haki ya kupiga kura kwa utaratibu ambao sheria itauweka.

“Serikali kupitia vikao vya Bunge la Febuarari 2024 iwasilishe muswada wa sheria itakayosimamia uchaguzi wa Serikali za mitaa tofauti na ilivyo sasa, ambapo TAMISEMI ndio chombo chenye jukumu hilo,”amesema

Aidha amesema upo umuhimu wa mchakato wa katiba mpya kuanza ili kuleta suluhisho la kudumu la Demokrasia nchini Tanzania

Pia amesema Katiba ifanyiwe marekebisho kwa kuweka mfumo wa usaili wa Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi na Makamu wake, mswada wa sheria ya uchaguzi wa Rais, Ubunge na udiwani uweke kifungu kinachotoa haki kwa kupiga kura kwa utaratibu ambao sheria itauweka.

“Serikali kupitia vikao vya Bunge la mwezi Febuarari 2024 iwasilishe mswada wa sheria itakayosimamia uchaguzi wa Serikali za mitaa tofauti na ilivyo Sasa ambapo wizara ya Tamisemi ndio chombo chenye jukumu hilo”amesema