October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

‘Learn Basketball Skills With ZYBA’ kuendelea wiki ijayo

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online

PROGRAM maalum ya mafunzo ya muda mrefu ya mpira wa kikapu kwa vijana ya ‘Learn Basketball Skills With ZYBA’ yataendelea wiki ijayo kama ilivyopangwa awali katika ratiba.

Wikiendi hii mafunzo hayo yalishindwa kufanyika kutokana na sababu zilizo nje ya uwezo wa waandaaji ikiwemo hali ya hewa kutokuwa nzuri.

Mkurugenzi wa Taasisi hiyo, Aziz Salim ameuambia Mtandao wa TimesMajira kuwa, baada ya Jumamosi kushindwa kufanyika kwa mafunzo hayo, walipanga yafanyike jana lakini hali ya hewa haikuwa rafiki jambo lililofanya pia kushindwa kufanyika.

Amesema, panapo majaaliwa, mafunzo hayo yataendelea tena wiki ijayo kama ilivyopangwa kwani matarajio yao ni kuona mafunzo hayo yanakuwa na mafanikio makubwa pamoja na kuhakikisha wanafanikisha lengo lao la kusaidia vijana wanaopenda mchezo huo kukuza na kuendeleza zaidi vipaji vyao.

Abdulsamad Abdulrahim ambaye ni mwanzilinshi na Mwenyekiti wa ‘Association of Tanzania Oil & Gas Service Providers’ (mwenye suti) akifafanulia jambo kwa Balozi mdogo wa Oman Dkt. Ahmed Hamood Al-Habsi katika ufunguzi wa program ya maafunzo maalum ya mchezo wa kikapu kwa vijana.

“Tunashukuru katika siku ya ufunguzi muitikio ulikuwa mkubwa na tunatarajia utakuwa mkubwa zaidi siku za mbeleni licha ya kuwa mwishoni mwa wiki tulishindwa kuendelea kutokana na changamoto zilizo nje ya uwezo wetu hivyo ratiba yote ikiendelea wiki ijayo,” amesema kiongozi huyo.

Katika siku ya ufunguzi wa programu hiyo, mgeni Rasmi Abdulsamad Abdulrahim ambaye ni mwanzilinshi na Mwenyekiti wa ‘Association of Tanzania Oil & Gas Service Providers’ aliahidi kutoa shiling Milioni mbili(2) kwa lengo la kuendelea kuwasaidia vijana katika kuendeleza vipaji vyao.

Mbali na kutoa ahadi hiyo ya fedha lakini pia aliahidi kusaidia zaidi siku za mbeleni huku Balozi mdogo wa Oman Dkt. Ahmed Hamood Al-Habsi akisema atatoa ushirikiano wowote utakaohitajika katika jitihada za kukuza na kuendeleza vipaji vya vijana.