April 29, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kunenge: Rais ametoa tani 300 za chakula waathirika wa mafuriko

Na Mwandishi Wetu, Timesmajiraonline,Pwani

MKUU wa Mkoa wa Pwani, Alhaj Abubakar Kunenge amepokea misaada ya Tan 300 za unga ,mchele na maharage kutoka kwa Rais Samia Suluhu Hassan.

Kunenge alimshukuru Rais Samia kwa kuendelea kutoa msaada ili kuodokana na changamoto ya mafuriko Mkoani humo.

“Tumepokea tan 100 za maharage, tani 100 za mchele na tani 100 za maharage kutoka kwa Rais wetu Samia, tunamshukuru sana kwa msaada huu ambao anaendelea kutoa , tumeshapokea tani 32 za mchele na nyingine zipo njiani,” alisema.

Alieleza kuwa hadi sasa katika tatizo hilo lililojitokeza kuna kambi saba zenye wananchi 749 kwa wilaya za Kibiti na Rufiji.

Kunenge alieleza kuwa waathirika wengine wamehifadhiwa kwa ndugu jamaa na marafiki. Alieleza kuwa makambi yameimarika na kuna huduma zote muhimu zinapatikana.

Kuhusu elimu kwa wanafunzi, alisema wameweka utaratibu mzuri wa wanafunzi kupata elimu na mafunzo kufidia muda ambao hawakusoma.

Pamoja na hayo alitoa tahadhari kwa wananchi kuacha kutumia mitumbwi kwenye maeneo yenye mafuriko kwani maji yanakasi kubwa.

Pia aliwaasa wananchi kuwa eneo hilo lina mamba na nyoka wa kubwa, hivyo waendelee kuchukua tahadhari.

Mkoa wa Pwani unaendelea kupokea misaada mbalimbali kutoka kwa wadau, ambapo pia April 14 Ofisi ya Waziri Mkuu ilitoa tani 31 za Unga kwa waathirika wa mafuriko Kibiti na tani 64 kwa Wilaya ya Rufiji sanjali na mahema saba na magodoro 157.