May 16, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kuelekea miaka mitatu, Rais Samia mwanamke anayejiami, aliyefungua uwanja huru kisiasa

Na Mwandishi Wetu, TimesMajira Online

SERIKALI ya Awamu ya Sita inaelekea kutimiza miaka mitatu chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, tangu aliporithi mikoba ya Hayati Rais John Magufuli, Machi 19, 2021.

Kwa muda huo wote wa  uongozi wa Rais Samia, tumeshuhudia utendaji, sera na falsafa yake ya R4 inavyozidi kushamirisha demokrasia nchini.

Kwenye uwanja wa siasa ameendelea kuachia nafasi nzuri wanasiasa kujadiliana na kuamua hatima ya maisha yao kisiasa, sanjari na kuruhusu pia waandamane, kuandamana jambo ambalo ni tofauti na ilivyokuwa huko nyuma.

Mfano, leo hii tayari tumeshuhudia chama kikuu cha upinzani CHADEMA kikifanya maandamano katika mikoa mitatu mikubwa nchini ya Dar es Salaam, Mwanza na Mbeya ambayo yalifanyika juzi.

Kinachoonekana leo kinanikumbusha kauli ya Rais Samia aliyoitoa siku za mwanzo aliposhika nafasi hiyo, akisema;  

“Nilisema mwanamke ni kujiamini nami kama Mwenyekiti wa CCM najiamini, najiamini kufungua uwanja wa siasa nikijua kwamba wana CCM tutakwenda pamoja na tutajadiliana na wenzetu na kuifanya nchi yetu twende vizuri.”  

Hicho alichokisema Rais Samia ndicho kinaonekana sasa, kwani kwenye maandamano  yanayofanywa na CHADEMA, tumeshuhudia  viongozi wa CHADEMA hicho kwamba kwenye maandamano yao hakuna hata sisimizi aliyeumizwa.

Maandamano hayo wanayojifunia hata sisimizi kutoumizwa  yameruhusiwa na Rais Samia tangu Serikali ya awamu ya tano ilipoyazuia pamoja na  mikutano ya hadhara mwaka 2016.

Tofauti ya sasa na wakati ule wa zama za hayati Magufuli ni kwamba utawala ule haukujali kuufungamanisha uhalali wa serikali yake katika mageuzi ya kidemokrasia.  Kitu ambacho Serikali ya Samia inajali hilo.

Kinachoonekana sasa ni kuendelea kueleweka kwa dhana ya R4 za Rais Samia Suluhu Hassan kwa wadau wa demokrasia nchini baada ya msafara wa Naibu Waziri Mkuu, Dkt. Doto Biteko kukutana na maandanano ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), huku kila upande ukiendelea safari zake bila kubughudhi mwenzake.