March 7, 2026

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kange aahidi kushughulikia miundombinu Nyamanoro akishinda Udiwani 

Judith Ferdinand, Timesmajira Online-Mwanza 

Mgombea Udiwani wa Kata ya Nyamanoro kupitia Chama Cha Mapindizi(CCM), jimboni Ilemela Abdulrahman Kange,ameahidi kushughulikia changamoto ya miundombinu ya barabara endapo atashinda katika uchaguzi mkuu unaotarajia kufanyika Oktoba 29,2025.

Kange amezungumza hayo Oktoba 4,2025,katika uzinduzi wa kampeni wa CCM Kata ya Nyamanoro jimboni Ilemela, uliofanyika sokoni Kariakoo mtaa wa Mnyampala,jijini Mwanza.

Mgombea Udiwani wa Kata ya Nyamanoro jimboni Ilemela mkoani Mwanza kupitia Chama Cha Mapindizi(CCM), Abdulrahman Kange,(kushoto), akinadiwa mbele ya wananyamanoro na MNEC Jamal Babu,katika mkutano wa uzinduzi wa kampeni wa chama hicho kwa Kata hiyo uliofanyika sokoni Kariakoo mtaa wa Mnyampala jijini Mwanza

Ambapo amesema Kata Nyamanoro ina mahitaji mengi lakini hitaji muhimu ni miundombinu ya barabara ambayo kwa sasa ni mibovu na changamoto kwa wananchi na ikizingatiwa  jiografia ya kata hiyo asilimia 74.6 eneo lake ni milima yenye mawe.

Amesema,maana yake ni kwamba wakazi wengi wa Nyamanoro wapo milimani na Kata hiyo ina wakazi wasiopungua 24,642 kati yao wanaume 11,751 na wanawake 12,873 na kaya zisizopungua 7,357,hivyo kazi anayoiomba anaijua.

“Nikipewa ridhaa na kuwa Diwani kwa miaka mitano nitashughulikia  changamoto hiyo kwani jambo la kwanza wananyamanoro wanahitaji barabara,jambo la pili wananyamanoro wanahitaji barabara na jambo la tatu wananyamanoro wanahitaji barabara,” amesema Kange na kuongeza:

“Miundombinu yetu ndani ya Kata ya Nyamanoro ni mibovu,hii barabara ya hapa tunapofanyia mkutano sokoni Kariakoo ina miaka 15 haijafanyiwa marekebisho.Ninaomba ridhaa kwenu ya kuwa mtumishi  na  tutaenda kufanya kazi kwa pamoja na barabara zitapatikana na kupitika,”.

Mgombea Udiwani wa Kata ya Nyamanoro jimboni Ilemela mkoani Mwanza kupitia Chama Cha Mapindizi(CCM), Abdulrahman Kange, akizungumza na wananchi wa Kata hiyo hawapo pichani katika uzinduzi wa kampeni ya chama hicho, uliofanyika sokoni Kariakoo mtaa wa Mnyampala jijini Mwanza

Sanjari na hayo amesema,kipande cha barabara cha kilomita 2 kutoka Kona ya Bwiru hadi Kilimahewa,atashirikiana na Mbunge anayetokana na CCM kuhakikisha linajengwa kwa kiwango cha lami ili kumsaidia  kutekelezwa ahadi ya mgombea kiti cha Urais kupitia chama hicho Dkt.Samia Suluhu Hassan,aliyoitoa kwa wananyamanoro.

Kwa upande wake mmoja wa wananchi wa Kata Nyamanoro,Agnes Lucas,ameridhishwa na ahidi zilizotolewa na mgombea Udiwani wa Kata hiyo kupitia CCM hasa ya miundombinu ya barabara.

Amesema,endapo mgombea huyo atavitekeleza kwa asilimia 100, Kata hiyo itafunguka na kuwa na maendeleo zaidi usafiri na usafirishaji wa bidhaa utarahisishwa.

Baadhi ya wananchi na wanaCCM wa Kata ya Nyamanoro,waliohudhuria uzinduzi wa kampeni wa CCM Kata hiyo ulifanyika sokoni Kariakoo mtaa wa Mnyampala jimboni Ilemela jijini Mwanza