October 3, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Kampeni “Tuwaambie kabla hawajaharibiwa”yazinduliwa Rukwa

Na Israel Mwaisaka, Timesmajira Online,Rukwa

JESHI la Polisi mkoani Rukwa,limezindua kampeni ya “Tuwaambie kabla hawajaharibiwa ” yenye lengo la kuwalinda vijana dhidi ya changamoto mbalimbali,zinazoweza kuathiri fikra na tabia zao.Uliofanyika wilayani Nkasi.

Akitoa taarifa juu ya mpango huo,Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa ( SACP) Shadrack Masija,amesema kuwa, mpango huo umelenga kuwa msingi wa kuzuia vitendo vya ukatili na unyanyasaji katika jamii ya Tanzania,pamoja na kuwajenga kiakili na kitabia Ili waweze kuepuka athari mbaya za mazungira wanayokutana nayo.

Amesema,pia imelenga zaidi kuwasaidia wanafunzi waliopo shule za sekondari,vyuo vya kati na vyuo vikuu, ili wawe na uwezo wa kukabiliana na changamoto zinazowakumba, wanapoanza masomo yao.

Kwani atika umri huo ukutana na mabadiliko mbalimbali ya kimwili,hivyo kampeni hiyo itasaidia kupunguza mihemko ya vijana.

Akizindua kampeni hiyo,Mkuu wa Wilaya ya Nkasi,Peter Lijualikali,amesisitiza umuhimu wa kushirikiana na Jeshi la Polisi ,kupitia kamisheni ya Polisi Jamii na Dawati la Jinsia na Watoto.Huku akiwataka wanafunzi na wazazi,kuunga mkono jitihada hizo,ili malengo yafikiwe ya vijana wote wanakua salama.

Amesema kuwa Serikali,imekuwa katika jitihada mbalimbali za kuwalinda vijana na watoto kwa kutunga sheria ,hivyo kampeni hiyo inakwenda kuongeza chachu ya mapambano hayo.

Awali Mkuu wa Dawati la Jinsia na Watoto,Mrakibu Msaidizi wa Polisi (ACP) Faustina Mwakapangala,amesema kampeni hiyo,itakuwa chachu ya mabadiliko katika jamii,kwa kuwajenga wanafunzi na vijana ujasiri wa kukabiliana na changamoto na kuleta matokeo chanya kwa vizazi vijavyo.

Aidha Mkuu wa Dawati la Jinsia na Watoto Wilaya Nkasi Mkaguzi Msaidizi wa Polisi Atupele Mwakaliku pamoja na Ofisa wa Polisi Jamii Mkoa Rukwa, Kamishna Msaidizi wa Polisi Zacharia Bura,walisema kuwa vita hiyo ni kubwa, lakini itakua nyepesi kama kila mmoja katika nafasi yake atawajibika ipasavyo.

“Kuondoa ukimya kwa vijana,na kuwaambia ukweli, vitu wasivyostahili kuvifanya katika umri wao,bali wasubiri wakati wao, hivyo vijana watakuwa salama na kuzifikia ndoto walizonazo katika maisha yao,”.