October 6, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Mkuu wa wilaya hiyo, Jokate Mwegelo akihutubia. (Picha na David John).

Jokate: Wenye nia ovu msithubutu kuijaribu Kisarawe,tupo imara sana

Na David John, TimesMajira Online

Wakati nchi ikielekea kwenye Uchaguzi Mkuu unaotarajia kufanyika Oktoba 28,mwaka huu, Halmashauri ya Wilaya ya Kisarawe mkoani Pwani imeapa kutovumilia vitendo vya aina yoyote vya uvunjifu wa amani na haiko tayari kukubali kujaribiwa.

Hivyo imewataka wananchi wote kwa ujumla kuwa sehemu ya kuhakikisha wilaya hiyo inakuwa salama wakati wote, kwani bila ya amani hakuna maendeleo, hivyo ni wajibu wa kila mwananchi kuifanya Kisarawe inakuwa salama muda wote.

Akizungumza wilayani Kisarawe wakati wa akifungua mafunzo ya vijana wa jeshi la akiba (mgambo)Mkuu wa wilaya hiyo, Jokate Mwegelo amesema, wananchi wote wanafahamu nchi inaelekea kwenye uchaguzi mkuu, hivyo ni kipindi ambacho wilaya hiyo kupitia Kamati ya Ulinzi na Usalama imejipanga vema kuhakikisha uchaguzi unafanyika kwa amani.

“Nimekuja kufungua mafunzo haya ya jeshi la akiba, nikiamini kuwa tunakwenda kuanda vijana wazalendo kwa nchi yetu, vijana ambao watakuwa tayari kuhakikisha hawashiriki kwenye matukio ya uvunjifu wa amani.Tena kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi mkuu huwa kuna vitendo vinavyoashiria kuvuruga amani.

“Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Kisarawe yote iko hapa, na kwa niaba yao naomba nieleze wazi, tumejipanga na hatutakuwa tayari kujaribiwa na mtu yoyote.Hivyo ni ombi langu kwenu ninyi vijana pamoja na vijana wengine wote wa Kisarawe na wananchi kwa ujumla tuwe wamoja kwa kuifanya Kisarawe yetu kuendelelea kubaki salama,”amesema Jokate.

Washiriki wa mafunzo ya mgambo wilayani Kisarawe. (Picha na David John).

Amesisitiza kuwa, hawatacheka na mtu yoyote atakayefanya vurugu na hawatasita kumshughulikia.”Kipindi hiki cha uchaguzi, ni kipindi muhimu na sisi tuko vizuri na yoyote atakayejihusisha na vurugu,uvunjifu wa amani hatavumiliwa kwani bila amani hakuna majigambo mengine yoyote.”

Ameomba vijana hao wapapato 150 walioko mafunzoni kuwa sehemu ya raia wema ambao watasaidia wilaya ya Kisarawe kuhusu mtu, kikundi ama watu ambao wanapanga kufanya vurugu au matukio yoyote ya kihalifu, na kwamba hicho kitakuwa moja ya kipimo chao.

Pia amesema watakapokuwa wakirejea majumbani wa kawe sehemu ya kutoa elimu kwa jamii kuhusiana na kujiepusha na vitendo visivyovumulika.

Wakati huo huo amesema ni vema vijana kuhakikisha wanashiriki kikamilifu kuchagua viongozi wao kuanzia ngazi ya diwani, mbunge na Rais na hivyo kila mmoja atunze kitambulisho chake cha kupigia kura, kwani vijana wengi huwa wanauza vitambulisho jambo ambalo si sawa kwani wana umuhimu wa kuchagua kiongozi wao wanayemuhitaji.

Kwa upande wake Mshauri Jeshi hilo la Akiba Wilaya ya Kisarawe, Meja Mohamed Wawa amesema kuwa, mafunzo hayo yalianza tangu Julai 13, mwaka huu na yatakuwa ya miezi minne ambapo wanategemea kumaliza Novemba 2, mwaka huu kama hakutakuwa na mabadiliko.