October 1, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

IRUWASA yajivunia mafanikio kwenye TEHAMA ufungaji mita za malipo ya kabla

Na Zena Mohamed,Timesmajiraonline,Dodoma.

MAMLAKA ya Maji safi na Usafi wa Mazingira Mkoa wa Iringa (IRUWASA)yajivunia mafanikiwa katika eneo la TEHAMA kwa kufunga mita za malipo kabla (prepaid water meters) kwa wateja 6,752 na kuwa Mamlaka inayoongoza nchini kwa kufunga mita nyingi za maji za malipo kabla.

Hayo yamesemwa jijini hapa leo,Februari 27 ,2023 na Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka hiyo Mhandisi David Pallangyo wakatu akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mafanikio na  utekelezaji wa shughuli za mamlaka hiyo.

Mha.Pallangyo amesema kuwa ufungaji wa mita  hizo za maji zimesababisha kwa kiwango kikubwa watumiaji wa maji kuondokana na malalamiko ambayo walikuwa wakiyalalamikia hapo awali.

“Mamlaka imejitahidi kuhakikisha inafunga mita za malipo kabla kwa wanachi pamoja na baadhi ya taasisi jambo ambalo kwa kiasi kikubwa zimesaidia kupunguza malalamiko, na kuwafanya watumiaji kuamini kuwa wanachokitumia ni sahihi na wala hawaibiwi,

“Mamlaka inaendelea kuboresha miundombinu ya upatikanaji wa maji ya kutosha sambamba na kushirikiana na wadau mbalimbali katika kulinda vyanzo vya maji ili kuondokana na uharibifu wa mazingira jambo ambalo linaweza kusababisha maji kuwa ya shida” amesema.

Aidha  Pallangyo  ameeleza kuwa kiasi cha sh. bilioni 2 zimetengwa kwa ajili ya miradi ya maji ya IRUWASA ambapo fedha hizo zitasaidia kuhakikisha miradi ya maji inaendelea kuimarika na kuwafanya wakazi wa mkoa kuondokana na tatizo la maji.

Amesema kuwa katika kutekeleza miradi hiyo pia itasaidia kupatikana kwa ajira zaidi ya 6400 za mikataba na kuongeza pato  la mtu mmoja mmoja na taifa huku kila mmoja akiwa na shahuku ya kufanya kazi kwa lengo la kujikwamua kiuchumi.

Vilevile Mha.Pallangyo ameeleza kuwa IRUWASA imeweza kuvuka lengo la sera ya Maji na Ilani ya Chama tawala ya kutoa huduma ya usambazaji maji kwa mji wa Iringa na maeneo ya pembezoni inayowafikia wakazi hao kwa asilimia 97.

Pia amesema IRUWASA imefanikiwa kuhakikisha huduma ya maji Mjini Iringa na maeneo ya pembezoni inapatikana kwa wastani wa saa 23 kwa siku.

“IRUWASA imefanikiwa kuongeza ukusanyaji maduhuli (revenue collection) kwa huduma zilizotolewa kutoka wastani Tshs 770M/= (2020) kwa mwezi hadi 860M/= (2023) hivyo hali hii inaiwezesha IRUWASA kuweza kugharamia kwa kiasi kikubwa uendeshaji wa Taasisi,”amesema.

Pamoja na hayo amesema IRUWASA  imefanikiwa kupunguza kiasi cha maji yasiyolipiwa (NRW) kwa upande wa Iringa Mjini kutoka wastani wa 24.6 (2020) hadi wastani wa 22.52% ,mwezi Desemba, 2022 

huku idadi ya wateja/maunganisho ya Majisafi imeongezeka kutoka 28,133 (2020) hadi 40,549 (Desemba, 2022).