May 13, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

IAA yaunga mkono jitihada za elimu ya Samia Scholarship

Na Penina Malundo

CHUO cha Uhasibu Arusha (IAA), kimeunga mkono Samia Scholarship kwa kutangaza rasmi utoaji wa ufadhili wa masomo katika kozi tano ikiwemo Kozi ya ngazi ya Shahada ya kwanza ya fani za fedha, ukaguzi wa hesabu, usimamizi wa mikopo, media anuwai na mawasiliano kwa umma, ukutubi na usimamizi wa nyaraka.

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam na Mkuu wa Chuo hicho, Prof. Eliamani Sedoyeka, wakati akiongea na waandishi wa habari alisema IAA imeona ni jambo jema kuunga mkono jitihada ya Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan katika sekta ya Elimu hususani katika Samia Scholarship.

Amessema mbali na kuunga mkono huo pia ufadhili huo ni kuondoa vikwazo vya kifedha kwa wanafunzi na kutoa fursa sawa kwa kila atakayekidhi vigezo kusoma kozi hizo.

“Rais Samia kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia mwaka huu ametoa udhamini wa masomo kwa wanafunzi wa masomo ya sayansi maarufu kama Samia Schokarship hivyo siisi kama taasisi ya elimu ya juu tumeamua kuunga mkono juhudi hizo kuamua kutoa elimu bure kwa kozi hizo,”amesema.

Sedoyeka amesema udhamini huo utawalenga wahitimu wa kidato cha sita kwa mwaka 2022 na 2023 wenye ndoto na malengo ya kusoma kozi hizo wanaokabiliwa na changamoto za kifedha.

“Ili muombaji akidhi vigezo vya kupata udhamini huu ni lazima awe ameomba kujiunga na chuo chetu na kufanya udahili nawakaribisha wahitimu wote wenye sifa kujiunga na chuo chetu kwa ngazi ya shahada ya kwanza katika maeneo tajwa,”amesisitiza.

Amesema kupitia ufadhili huo wanatarajia kuona mafanikio makubwa kwa wanafunzi hao katika kufikia malengo yao ya kielimu na kuchangia katika maendeleo ya jamii na taifa kwa jumla.

Prof.Sedoyeka amesema elimu ni msingi wa Maendeleo katika jamii na nchi kwa ujumla,kutokana na kutambua Changamoto zinazowakabili vijana wengi katika kufikia elimu Bora hivyo IAA imeamua kusaidia vijana katika kutoa ufadhili huo.

“Baadhi ya vijana wetu wenye vipaji na Hamasa ya kusoma wanakumbana na vikwazo vya kifedha ambavyo vinaweza kuwa kikwazo cha kufikia malengo yao ya elimu,”amesema na kuongeza

“Tumeamua kuchukua hatua mbele kwa kuanzisha programu hii ya udhamini wa masomo,”amesema.