May 7, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Gambo ahoji wamachinga kutopewa vitambulisho

Na Nasra Bakari, TimesMajira Online

MBUNGE wa Arusha Mjini, Mrisho Gambo ameitaka Serikali kuwapatia vitambulisho baadhi ya wamachinga ambao hawatambuliki serikalini kwani bado wanaendelea kuchajiwa ushuru katika Halmashauri ya mkoa huo.

Akizungumza jana Bungeni Mkoani Dodoma katika kipindi cha maswali na majibu, Gambo alisema, wamachinga wapo wengi katika jiji la Arusha ambao wamekosa maeneo ya kufanyia biashara na baadhi yao ndiyo wametambulika na Serikali na wamepatiwa vitambulisho, lakini waliobaki bado wanachajiwa ushuru.

Alisema, taarifa iliyotolea na Naibu Waziri inatuambia kwamba wamachinga 5,426 ndiyo ambao wanatambuliwa na Serikali vitambulisho vimetolewa kwa wamachinga 1,187.

“Je ni kwanin wamachinga waliobaki mpaka sasa hivi hawajapatiwa vitambulisho na wanaendelea kuchajiwa ushuru katika halmashauri ya Arusha?” Alihoji Mbunge Gambo.

Swali hilo lilijibiwa na Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Festo Dugange akisema; ”Nimuhakikishie Mbunge kwamba taarifa hizi zimetoka ndani ya Halmashauri ya jiji la Arusha kwa watendaji wa Serikali ambao wamejiridhisha na idadi ya wamachinga waliopo mbali na idadi ya wamachinga waliopewa vitambulisho.

Dugange alisema, pamoja na kwamba serikali la jiji la Arusha lilikuwa katika mpango wa kuwapanga wamachinga lakini utaratibu wa kutoa vitambulisho ulikuwa unaendelea sambamba na kuwapanga wamachinga kwahiyo naomba nikutoe hofu katika hilo.

“Na kuhusiana na hilo kwamba kwanini mpaka leo baadhi ya wamachinga hawajapata vitambulisho, jambo hilo ni swala la kutoa elimu na kuhamasisha kwa baadhi ya wamachinga wasiokuwa na uelewa,” alisema na kuongeza.

Alisema, elimu itatolewa kwa baadhi ya wamachinga wasiokuwa na uelewa ili waweze kuvipata vitambulisho hivyo na kazi hii itaendelea siku hadi siku kwa watu mbalimbali ili kuwaelimisha.