June 26, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

EWURA yatoa msaada wa vifaa tiba hospitali ya Wilaya ya Nyamagana kupitia fedha za CSR

Na Judith Ferdinand, Times Majira online , Mwanza

Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji(EWURA),imetoa msaada wa vifaa tiba vyenye thamani ya zaidi ya milioni 5, kwa hospitali ya Wilaya ya Nyamagana (Butimba) kupitia fedha za kurejesha huduma kwa jamii(CSR).

Akizungumza katika kikao cha tano cha Baraza la kwanza la Wafanyakazi wa EWURA kilichofanyika jijini Mwanza, Mwenyekiti wa kikao hicho Poline Msuya, ameeleza kuwa EWURA imekuwa na utaratibu wa kufanya kitu kwa jamii kila pale inapowezekana kufanya.

Msuya ameeleza kuwa kama sehemu ya kutambua jitihada za Serikali ya awamu ya sita hususani katika sekta ya afya, EWURA imeona vyema kutoa msaada wa vifaa tiba kwa hospitali ya Wilaya ya Nyamagana vyenye thamani ya milioni 5.24 (5,249,200).

Ambapo kiasia hicho kinalenga kugharamia mashine ya kupimia shinikizo la damu(BP Machine digital) 6 zenye thamani 426,000, viti vya magurudumu kwa ajili ya kusaidia wagonjwa(Wheel Chair) 2 vyenye thamani ya 709,000,vitanda vya uchunguzi (Examination Beds) 4 vyenye thamani ya 1,917,200 pamoja na vifaa vya kujifungulia(Delivery Kits) 10 vyenye thamani ya 2,197,000.

“Ni imani yetu kuwa mchango huu kwa hospitali utasaidia kuokoa maisha ya watanzania wenzetu na pia kuboresha huduma ya utoaji afya katika Mkoa wa Mwanza,”ameeleza Msuya.

Akizungumzia kikao hicho cha Baraza la la Wafanyakazi wa EWURA,Msuya ameeleza kuwani wajibu wao kuhakikisha upatikanaji wa huduma zinazodhibitiwa na EWURA, ambazo ni huduma za nishati na maji zinapatikana kwa wakati na kwa gharama nafuu.

“Katika kutimiza majukumu hayo, Baraza la Wafanyakazi ni moja ya nyenzo muhimu sana katika kuhakikisha malengo ya taasisi yanafikiwa,kwa kutumia chombo hiki tumezidi kuona mafanikio ya ushiriki wa wafanyakazi kwa uwazi katika kuleta mafanikio hadi hapa tulipofika,” ameeleza Msuya.

Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza Dkt.Sebastian Pima, akizungumza mara baada ya kukabidhiwa mfano wa Hindi kwa ajili ya kununulia vifaa hivyo ameishukuru EWURA katika kuunga jitihada za serikali kwenye sekta ya afya kwenye Wilaya hiyo.Dkt.

Pima ameeleza kuwa ameeleza kuwa ni hospitali kuwa ndani ya Jiji ya umma ukiondoa ya Rufaa ya Kanda ya Bugando na ya Mkoa ya Sekou-Toure,ambapo kwa mwezi inahudumia wamama wanaojifungua 650 hadi 750.Pia ameeleza kuwa kwa mwezi mmoja inahudumia wagonjwa wa nje 8000 mpaka 12,000 huku huduma za kliniki kwa mama wajawazito 3500 hadi 5000.

“Sisi hatujiendeshi kwa faida ya biashara sera ya afya inasema huduma kwa mama mjamzito ni bure,ingawa rasilimali hazitoshi tunaishukuru serikali yetu imekuwa ikituletea fedha na tumemaliza kujenga jengo la huduma ya wagonjwa wa nje,uhitaji wa wananchi unaongezeka kwa kasi,mchango wenu huu unaenda kupunguza uhitaji katika hospitali yetu ya Wilaya na kusaidia kabisa mwananchi aliyekusudiwa”ameeleza Dkt.Pima.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana Amina Makilagi akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza,ameipongeza EWURA kwa kuiunga mkono Serikali kwa vitendo kwa jambo hilo adhimu la kuchangia vifaa tiba katika hospitali hiyo ya Wilaya ya Nyamagana.

“Hiki mlichokifanya kwa kulenga kuimarisha huduma za afya katika jamii yetu ni jambo la kuigwa na kushukuru sana. Tunawashukuru sana,nikuombe Mganga Mkuu, misaada hii ilenge kuimarisha huduma kama ilivyokusudiwa,”ameeleza Makilagi.

Pia ametumia fursa hiyo kusisitiza wafanyakazi wa EWURA kuwa taifa linawategemea kufanya kazi kwa weledi na kasi ya juu kuleta unafuu wa utoaji wa huduma na zenye ubora kwa wananchi katika sekta ya nishati na maji.

Pia kuzingatia uwazi katika upimaji wa utendaji wa wafanyakazi na kuhakikisha utekelezaji wa majukumu unakwenda sanjari na thamani halisi (value for money) ya rasilimali zilizopo ili kutokuwepo manunguniko, ugomvi, chuki, husda na majungu mahali pa kazi, ambayo yasipodhitiwa hupelekea utendaji hafifu.

“Ninawasisitiza wafanyakazi kuwajibika ipasavyo katika utekelezaji wa majukumu yenu sanjari na kufuata maadili ya utumishi wa umma, kuwa na nidhamu, utii na heshima wakati wote wa utendaji wenu,”amesisitiza Makilagi.

Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza Dkt.Sebastian Pima,wa pili kulia akipokea mfano wa hundi kutoka kwa Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana Amina Makilagi wa pili kushoto kwa ajili ya kununulia vifaa tiba katika hospitali ya Wilaya ya Nyamagana iliyotolewa na EWURA kupitia fedha za CSR,huku wa kwanza kushoto ni Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa EWURA Poline Msuya,katika kikao cha Baraza hilo kilichofanyika jijini Mwanza.
Mkuu wa Wilaya ya Nyamagana Amina Makilagi akizungumza katika kikao cha tano cha Baraza la kwanza la Wafanyakazi wa EWURA kilichofanyika jijini Mwanza.
Mwenyekiti wa Baraza la Wafanyakazi wa EWURA Poline Msuya akizungumza katika kikao cha tano cha Baraza la kwanza la Wafanyakazi wa EWURA kilichofanyika jijini Mwanza.
Baadhi ya wajumbe walio hudhuria katika kikao cha tano cha Baraza la kwanza la Wafanyakazi wa EWURA kilichofanyika jijini Mwanza.