May 4, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Eng. Sanga akutana na kanisa la Anglikana kujadili changamoto ya uvamizi maeneo ya kanisa


Na Mwandishi wetu, TimesMajira Online, Dodoma


Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Eng. Anthony Sanga amehimiza maeneo ya Kanisa Nchini kuendelezwa na kulindwa kwa lengo la kuyalinda dhidi ya wavamizi na kuepukana na migogoro ya ardhi kwa siku za baadae.


Baba Askofu wa Kanisa la Anglikani Tanzania Maimbo Mdolwa amefika katika Ofisi za Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Mtumba Jijijini Dodoma mapema leo August 25, 2023 kwa ajili mazungumzo yanayohusu maeneo yanayomilkiwa na Kanisa hilo yaliyovamiwa na Wananchi katika sehemu mbalimbali hapa Nchini.


Katika mazungumzo yake na Kiongozi huyo mkubwa wa Kanisa Katibu Mkuu Sanga amesema wamekubaliana kuunda tume ya pamoja itakayopitia baadhi ya maeneo ya kanisa yenye changamoto ya migogoro ya ardhi ili kuyapatia ufumbuzi wa pamoja.


Aidha Katibu Mkuu Sanga amelitaja eneo la Kanisa hilo liliko Buza Wilayani Temeke kuwa sehemu ya kanisa hilo ambalo mara baada ya kuunda tume hiyo litafanyiwa kazi bila kuyataja maeneo mengine ya kanisa hilo yenye changamoto ya uvamizi kutoka wananchi wanaotaka kukalia eneo hilo bila kufuata taratibu zilizopo.


Wizara ya Ardhi ndiyo Wizara yenye dhamana ya kushughulikia masuala yote yanayohusia na Ardhi hapa Nchini na imekuwa ikipokea malalamiko ya wananchi wanao kabiliana na changamoto kama izo ikiwemo uvamizi wa ardhi na kujimilikisha maeneo hayo bila kuzingatia taratibu.