May 8, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

‘Elimu shirikishi muhimu kwa watu wenye ulemavu’

Na Penina Malundo,timesmajira,online

IMEELEZWA kuwa kuwepo kwa mpango binafsi wa elimu kwa watoto wenye mahitaji maalum baina ya wazazi na walimu utasaidia kwa kiasi kikubwa mtoto mwenye ulemavu kujifunza vitu vingi na kuvitambua.

Aidha, watoto hao wenye mahitaji maalum wakibadilishiwa mifumo yenye mazingira mazuri na salama itawafanya kuwepo katika elimu nzuri na jumuishi.

Hayo yalisemwa jana katika mkutano na waandishi wa habari kwa njia ya mtandao,Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika linalohudumia Watoto na Vijana wenye Mahitaji Maalum na Ulemavu, Noelah Msuya.

Amesema mpango huo unaandaliwa kwa mtoto husika ukiwa na malengo maalum ya mtoto nini anahitaji kufanikishiwa ,kujifunza kwa kipindi maalum.

Amesema mpango huo mara nyingi uandaliwa na Mwalimu akishirikiana na wazazi au walezi na unaweza kujumuisha watu wanaojitoa katika huduma za afya kwa.Watoto.

Msuya amesema shirika lao limekuwa likisaidia watoto wenye mahitaji maalum kuwa na uwezo wa haraka wa kutambua wenzao wakiwemo wenye ulemavu kujua anauhitaji gani kwa muda wowote.

“Shirika letu limekuwa litoa mafunzo juu ya elimu jumuishi kwa Watoto wenye mahitaji maalum na suala zima la watu wenye ulemavu katika ngazi mbalimbali ikiwemo kwa viongozi wa serikali tumekuwa tukiwafundisha suala la watu wenye ulemavu na mazingira yao,”Amesema

Kwa upande wake, Miriam Elisha amesema jamii inahitaji kuwa na elimu jumuishi kwa lengo la kuwaweka watu katika usawa na kutoa fursa sawa kwa watu wenye mahitaji maalum au watu wenye ulemavu.

Amesema elimu jumuishi ni njia moja wapo ya upungufu wa utegemezi katika jamii hususani kwa Watoto wenye mahitaji maalum.

“Mfano Watoto wenye ulemavu wa ufahamu wakipata madarasa yenye mwanga inaamsha akili zao,ila ukitaka atulie kila dakika 20 unapaswa kumpa mapumziko ili aweze kutuliza hisia zake,”amesema na kuongeza

“Walimu wenye ulewa na wanaojua matatizo ya usonji kwa Watoto hawapaswi kuona mzigo kuwafundisha Watoto hao bali wajue mbinu sahihi za kuwafundisha katika utambuzi wa vitu mbalimbali,”alisema

Aidha alisema ni wakati muafaka sasa kwa vyuo vikuu kuweza kuanzisha kozi maalum ya ufundishaji wa Watoto hao wenye mahitaji maalum ili kupata wataalamu watakaotumia mbinu mbalimbali za kuwafundishia.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Lukiza Autism,Hilda Nkabe amesema mafunzo hayo yaliyotolewa kwa wadau ni moja kati ya utekelezaji wa mradi wa inclusive media inayofadhiliwa na Internews.