October 8, 2024

Timesmajira

Gazeti Huru La Kila Siku

Elimu, muarobaini wa ajali mbalimbali

Na Daud Magesa, Timesmajira Online, Musoma

KAMANDA wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Mara, Augustine Magere,amesema mkakati wa kuzuia ajili,ni kuwekeza katika elimu kwa wananchi,wafanyabiashara wa vyombo vya usafirishaji,wavuvi na wachimbaji madini.

Huku akitoa tahadhari kwa wamiliki wa vyombo vya usafiri wa majini, kuzingatia uwezo wa vyombo vyao pamoja na wasichanganye watu,petroli na mizigo mikubwa.

Magere ametoa kauli hiyo, leo katika mahojiano na waandishi wa habari kuhusu mbinu na mikakati ya kuzuia majanga katika jamii yakiwemo ya moto,ajali za majini,barabarani na migodini.

Amesema wanatoa elimu ya kuzuia majanga kwa asilimia 75 kabla hayajatokea.Na hawapo kwa ajili ya kuzima moto,hayo ni matokeo ya dharura,wanazuia kwa kufanya ukaguzi na kushauri mamlaka husika na kazi ya uokozi ni asilimia 25.

“Kipaumbele ni kuwapa elimu wananchi wakielewa wanaweza kuzuia majanga yasitokee(limitional control),wawe na vifaa vya kuzima moto na utaalamu wa kuvitumia, ili kunusuru maisha ya watu hasa nyumbani,viwandani na kwenye vyombo vya usafirishaji kama magari,mitumbwi ama boti zilizogaguliwa,”amesema.

Sanjari na hayo,ameeleza matukio ya ajali za majini na migodini, zinasababishwa na jamii ya wavuvi na wachimbaji wa madini, kwa sababu wanafanya kazi kwa mihemko na mazoea bila kuzingatia sheria na usalama wao.

“Migodini wanatumbukia na kufukiwa na vifusi,mashimo,na kamba wanazotumia kushuka chini shimoni hazikaguliwi,na siyo imara pia hawana vifaa vya mawasiliano wala kubaini kama kuna maji shimoni,”.

Hata hivyo amewashauri wananchi kuchukua tahadhari majini,huku magari yakiwemo ya kusafirisha mafuta na abiria yawe na vifaa vya kuzima moto na watu wenye utaalamu wa kuvitumia, pamoja na sanduku la huduma ya kwanza.Magari yasijaze mafuta kwenye vitu yakiwa na abiria ndani.

“Changamoto ni watu kutofahamu namba 114 ya dharura, hii inasaidia kuepuka ucheleweshaji wa taarifa,ambao husababisha zimamoto kuchelewa kufika eneo la tukio kwa wakati,wengine wana hofu ya kutozwa gharama kwa huduma hiyo ambayo ni ya bure,”amesema Magere.

Kadhalika amewataka wananchi,kutoa taarifa za majanga kwa maelekezo sahihi na kuwataka watumiaji wa vyombo vya moto,kuacha tabia ya kuzuia magari ya wagonjwa na ya kuzima moto,kwani wanachelewesha shughuli za uokoaji.

Aidha ameeleza kuwa,changamoto ya ujenzi holela inachangia kuziba barabara za mitaa na kusababisha magari ya watoa huduma kushindwa kupita.Hivyo ameshauri wananchi wanapojenga nyumba waache nafasi ya miundombinu ya barabara.